2014-12-15 15:31:46

Gereza la Guantanamo kufungwa!


Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumatatu tarehe 15 Desemba 2014 amekutana na kuzungumza na Bwana John Kerry, katibu mkuu wa nchi wa Marekani mjini Vatican. Mazungumzo haya yamewahusisha viongozi waandamizi kutoka Ubalozi wa Marekani mjini Vatican pamoja na baadhi ya viongozi kutoka Sekretarieti ya Vatican.

Viongozi hawa kwa pamoja wamejadili kwa kina na mapana hali tete huko Mashariki ya Kati, vita na kinzani sehemu mbali mbali za dunia; umuhimu wa Israeli na Palestina kuanza tena majadiliano. Viongozi hawa wameangalia uwezekano wa Serikali ya Marekani kufunga gereza kuu la Guantanamo ambalo limekuwa ni mama wa kashfa nyingi za ukatili dhidi ya ubinadamu pamoja na kuangalia jinsi ambavyo Vatican inaweza kusaidia kupata suluhu ya kibinadamu kwa wafungwa walioko gerezani humo!

Kutokana na ufinyu wa muda, baadhi ya tema zimeachwa kiporo hadi wakati mwingine, ingawa viongozi hawa pia wamezungumzia vita na kinzani zinazoendelea kujitokeza huko Ucrain pamoja na janga la Ebola Afrika Magharibi.







All the contents on this site are copyrighted ©.