Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumatatu tarehe 15 Desemba 2014
amekutana na kuzungumza na Bwana John Kerry, katibu mkuu wa nchi wa Marekani mjini
Vatican. Mazungumzo haya yamewahusisha viongozi waandamizi kutoka Ubalozi wa Marekani
mjini Vatican pamoja na baadhi ya viongozi kutoka Sekretarieti ya Vatican.
Viongozi
hawa kwa pamoja wamejadili kwa kina na mapana hali tete huko Mashariki ya Kati, vita
na kinzani sehemu mbali mbali za dunia; umuhimu wa Israeli na Palestina kuanza tena
majadiliano. Viongozi hawa wameangalia uwezekano wa Serikali ya Marekani kufunga gereza
kuu la Guantanamo ambalo limekuwa ni mama wa kashfa nyingi za ukatili dhidi ya ubinadamu
pamoja na kuangalia jinsi ambavyo Vatican inaweza kusaidia kupata suluhu ya kibinadamu
kwa wafungwa walioko gerezani humo!
Kutokana na ufinyu wa muda, baadhi ya tema
zimeachwa kiporo hadi wakati mwingine, ingawa viongozi hawa pia wamezungumzia vita
na kinzani zinazoendelea kujitokeza huko Ucrain pamoja na janga la Ebola Afrika Magharibi.