Changamoto kwa wadau wa habari kutoka kwa Papa Francisko!
Wadau katika sekta ya mawasiliano ya jamii wanapaswa kutekeleza dhamana hii kwa kuwajibika
zaidi, kwa kujikita katika ukweli na uhuru; kwa kuijaza hadhira mambo msingi pamoja
na kuzingatia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.
Ni changamoto kubwa
inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipokutana na kuzungumza na wafanyakazi
wa Kituo cha Televisheni cha TV 2000 kinachomilikiwa na kuendeshwa na Baraza la Maaskofu
Katoliki Italia, Jumatatu tarehe 15 Desemba 2014.
Baba Mtakatifu anasema kwamba,
kwa bahati mbaya, mawasiliano ya jamii kwa kipindi kirefu yamejikita katika propaganda
kwa ajili ya masuala ya kisiasa, uchumi na uthibiti wa teknolojia. Jambo la msingi
ni kuhakikisha kwamba vyombo vya mawasiliano ya kijamii vinazungumza ukweli katika
uhuru unaoheshimu na kuzingatia namna na mahali pa kuufikisha ukweli huu. Wanahabari
wanapaswa kuasha tena uwezo wa watu kuwasiliana kikamilifu.
Vyombo vya mawasiliano
viwe ni kichocheo kinachopania kuwajaza watu mambo msingi katika maisha, kwa kuwasaidia
watu kufahamu kile kinachotangazwa, kwa kutoa nafasi kwa watu kufahamu mahudhui yanayokusudiwa
badala ya kuwapatia watu majibu ya mkato. Baba Mtakatifu anasema haya ni mawasiliano
ambayo yanafungua bila kufunga, kumbe, wanahabari hawana budi kumwachia nafasi Roho
Mtakatifu afanye kazi ya kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano kati ya watu.
Baba
Mtakatifu Francisko anawataka wadau wa habari kuhakikisha kwamba, wanazungumza na
mtu mzima: kiroho na kimwili kwa kujiepusha na "dhambi za waandishi wa habari" zinazojikita
katika kuwapaka watu matope; kueneza umbea na udaku pamoja na kutoa maamuzi katika
ukweli wa mambo. Mawasiliano yasiwe ni kwa ajili ya "kumlipua mtu" au kuwajengea watu
hofu! Mawasiliano ya namna hii yana walakini mkubwa.
Kumbe, kuna haja kwa
wadau wa habari kuhakikisha kwamba, wanazungumza na mtu mzima: kiroho na kimwili;
yote haya yanalenga pamoja na mambo mengine kujenga na kudumisha utamaduni wa watu
kukutana katika ulimwengu mamboleo. Hapa watu wajifunze kutoa na kupokea kutoka kwa
wengine.Baba Mtakatifu anawatakia kheri na baraka wafanyakazi wa Kituo cha Televisheni
cha Baraza la Maaskofu Katoliki Italia wanapojipanga upya ili kutekeleza wajibu wao
kikamilifu, ili kutoa huduma makini katika Kanisa.
Baba Mtakatifu anawashukuru
kwa ushirikiano mzuri uliopo kati yao na Kituo cha Televisheni cha Vatican, ili kuhakikisha
kwamba, Mafundisho ya Mababa wa Kanisa yanawafikia watu wengi zaidi. Anawashukuru
wafanyakazi hawa kwa weledi na upendo wao kwa Injili anawatakia wote Noeli Njema.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.