Barua kutoka kwa Papa Francisko kwa ajili ya wafungwa!
Kipindi cha kutumikia adhabu gerezani ni fursa kwa mfungwa kukua ili hatimaye, aweze
kupata amani na utulivu wa ndani na kwamba, kila mfungwa anapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa
utu wake. Kuna wafungwa wengi ambao wamemwandikia Baba Mtakatifu Francisko barua zinazoonesha
mateso na mahangaiko yao gerezani, pamoja na kumshirikisha siri za maisha yao.
Si
wakati wote Baba Mtakatifu amefaulu kuwajibu kwa wakati muafaka kutokana na sababu
mbali mbali. Katika kipindi hiki cha Majilio, Baba Mtakatifu Francisko amewaandikia
wafungwa wanaotumikia adhabu yao kwenye Gereza la Latina lililoko mjini Roma, barua
ambayo imekabidhiwa kwa Padre Nicola Cupaiolo, Mhudumu wa maisha ya kiroho kwenye
gereza hili, kwa lengo la kuwatakia kheri na baraka katika Maadhimisho ya Siku kuu
ya Noeli, Mwana wa Mungu anapozaliwa tena mioyoni mwa waamini.
Baba Mtakatifu
anawaalika wafungwa wanapotekeleza adhabu yao, kuutumia vyema muda huu kama changamoto
ya kukua na kukomaa, ili kuweza kupata amani na utulivu wa ndani, chemchemi ya maisha
na matumaini mapya kutoka kwa Mwenyezi Mungu; matumaini ambayo kamwe hayawezi kudanganya.
Anawapongeza
wafungwa ambao wanatumia nafasi hii kufanya hija ya maisha ya kiroho, kwa kushirikiana
na Padre Nicola Cupaiolo ambaye anawathamini na kuwaona kuwa ni ndugu na dada zake
katika Kristo si tu kutokana na wajibu wa kiofisi.
Baba Mtakatifu anawaalika
wafungwa kuendelea na hija hii ya maisha ya kiroho pasi na kukata tamaa na kwamba,
anawashukuru wadau mbali mbali wanaoendelea kuwasaidia wafungwa katika mchakato wa
kujiletea mabadiliko makubwa katika maisha. Baba Mtakatifu anapenda kuwazawadia Misale
Mpya ya Altareni itakayowasaidia kugundua njia mpya ya maisha kwa kushikamana na Yesu
Kristo katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu. Yesu ni mganga mahiri wa
madonda na machungu yao ya ndani; ni rafiki mpendelevu anayeambatana nao katika maisha
ya kila siku, kwa kuwapatia chakula kilichoshuka kutoka mbinguni kwa ajili ya wokovu
wao sanjari na nguvu ambayo haiwezi kuzuiwa na kuta za gereza.
Baba Mtakatifu
Francisko anawaombea wafungwa ili waweze kufarijiwa na Kristo mwenyewe kwa kuwapatia
amani na uwepo wake mwanana! Anasali kwa ajili yao binafsi, ndugu na jamaa bila kuwasahau
wadau mbali mbali wanaotoa huduma gerezani hapo!