2014-12-13 15:24:56

Papa Francisko, Hongera kwa Daraja la Upadre!"Besi Dei" ni tarehe 17 Desemba!


Daraja Takatifu ni Sakramenti ambayo kwayo utume uliokabidhiwa na Kristo kwa mitume wake huendelea kutekelezwa katika Kanisa hadi mwisho wa nyakati. Hii ni Sakramenti ya huduma ya kitume ambayo ina ngazi kuu tatu: Uaskofu, Upadre na Ushemasi.

Baba Mtakatifu Francisko anapojiandaa kuadhimisha Siku yake ya kuzaliwa hapo tarehe 17 Desemba, Jumamosi tarehe 13 Desemba 2014 amefanya kumbu kumbu ya siku ile alipopewa Daraja Takatifu la Upadre tarehe 13 Desemba 1969 baada ya kuhitimu masomo na majiundo yake ya Kikasisi, huko Argentina. Baba Mtakatifu katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii, anawaalika kuendelea kumwombea katika maisha na utume wake.

Kunako mwezi Juni 1992 aliteuliwa na Mtakatifu Yohane Paulo II kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Buenos Aires, Argentina. Kunako mwaka 1998 akateuliwa kuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires. Na kunako mwaka 2001 akateuliwa na Mtakatifu Yohane Paulo II kuwa Kardinali. Kunako tarehe 13 Machi 2013 akachaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.







All the contents on this site are copyrighted ©.