Baba Mtakatifu ameonyesha ukaribu wake na kuwafariji Wakristo wengi wanaoishi katika
mazingira magumu na hatarishi , hasa Syria na Iraq, ambako wanakabiliwa na unyama
wa magaidi unao washinikiza Wakristo kuihama nchi yao. Papa ameonyesha hisia zake
wakati akikutana na jumuiya ya Wakatoliki wa Syria ya Antokia , waliokusanyika hapa
Roma, kwa ajili ya Mkutano wa Sinodi yao , ambayo imelazimika kufanyika nje ya nchi
yao kutokana na uwepo wa vita na madhulumu mengi kwa jamii ya Wakristo nchini humo.
Ujumbe huo ulikutana na Papa ukiongozwa na Patriaki Ignace Youssif III Younan, wa
Kanisa Katoliki la Syria.
Kiini cha hotuba ya Papa kwa wageni wake hasa kililenga
katika hatma ya jamii ya Kikristo Mashariki ya Kati. Alisema, kupitia kwao anaipaza
sauti yake kwa jamii yao iliyotawanyikia duniani kote. Papa alitoa ujumbe wa kutia
moyo, nguvu mpya ya kuishikilia imani yao , hasa kwa namna ya kipekee , Wakristo
wa Iraki na Syria , daima waendelee kuweka tumaini lao kwa Bwana, wakati huu mgumu
wa mateso na majaribu makubwa yanayowajengea hofu katika uso wa ghasia.
Sinodi
Kanisa Katoliki la Syro, imefanyika kwa nia kuu ya kupata majibu katika mahitaji
ya haraka ya kanisa, ambalo liko katika majaribu makubwa ya kiroho kwa waamini. Sinodi
kwa namna ya kipekee, pia imefanya mchakato kwa ajili ya kufanya mageuzi katika Liturujia
Takatifu , kama hatua mpya ya kuleta mwamko zaidi katika kupenda ibada. Kazi hii
, Papa alisisitiza, inalazimu kuwa na tafakari za kina kwa ajili ya kupata utambuzi
wa kutosha juu ya mila na desturi, kwa ufahamu kwamba, waamini wanajali unyeti
wa zawadi ya Neno la Mungu ukuu wa Ekaristi.
Papa alionyesha kutambua hali
ngumu katika Mashariki ya Kati, inayo sababisha na inaendelea kusababisha mabadiliko
katika kanisa, waamini wake wengi , wakilazimika kwenda kuishi ugenini, hali inayotoa
haja ya kuwa na mitazamo mipya ya kichungaji .
Papa amesema katika hali hiyo,
mna changamoto mbili zilizofungamana. Kwa upande mmoja, ni kuwa aminifu katika asili
yake; na kwa upande mwingine, ni kuwa na mchakato katika kazi za kichungaji kwenye
mwingiliano wa asili ya tamaduni mbalimbali katika kukidhi huduma ya Kanisa na mazuri
ya kawaida. Uhamaji huu wa waamini kuelekea mataifa mengine ni wazi hudhoofisha uwepo
wa Wakristo Mashariki ya Kati, nchi ya manabii, wahubiri wa kwanza wa Injili na nchi
ya mashahidi na watu wa Mungu wengi. Yote hayo alisisitiza Papa , yanahitaji uwepo
wa Wachungaji na waamini jasiri, walio imara katika kushuhudia Injili kulingana na
nyakati , jambo ambalo wakati mwingine si rahisi, kukabiliana na watu wa makabila
tofauti na dini tofauti.
Papa aliendelea kuonyesha utambuzi kwamba, wengi wamekimbia
na kutafuta hifadhi katika maeneo yaliyo salama zaidi , wamekimbia ukatili na unyama
unaofanywa dhidi yao kwa sababu ya imani yao, wametoka katika nyumba zao bila ya kuwa
na chochote hata kujua jinsi watakavyojikimu. Papa amewatia moyo kwamba wasikate
tamaa Kanisa katika umoja wake kama mwili wa Bwana, linatembea nao katika mateso yao
, kwa kujaribu kuratibu juhudi za kukabiliana na mahitaji ya kibinadamu ya wote wale
ambao kubaki nyumbani, wote wale waliokimbilia nchi nyingine. Papa Francisco
mwisho alihimiza Kanisa Katoliki Syria, liendelee na huduma yake kwa matumaini,
huduma kwa jumuiya hii ya zamani ya Kikristo.