2014-12-12 13:58:42

Mwanadamu apewe kipaumbele cha kwanza katika mikakati ya maendeleo!


Jumuiya ya Kimataifa tangu mwaka 2008 ilijiwekea mikakati ya kupambana na baa la umaskini miongoni mwa watu, ili kufikia mwaka 2017, baa hili liweze kupewa kisogo na Jumuiya ya Kimataifa kwa watu kuwa na maisha bora zaidi. RealAudioMP3

Ni katika mwelekeo huu wa kupambana na vizingiti vinavyokwamisha maendeleo ya mwanadamu, Jumuiya ya Kimataifa ikajiwekea Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015, mwaka mmoja tu kuanzia sasa.

Takwimu zinaonesha kwamba, kumekuwepo na mafanikio katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia, hata hivyo Jumuiya ya Kimataifa haina budi kujifunga kibwebwe kwani bado kuna changamoto nyingi zinazopaswa kufanyiwa kazi, ili kuondokana kabisa na baa la umaskini wa hali na kipato duniani. Ili kweli watu wengi waweze kupata mafanikio makubwa katika maisha, kuna haja ya kuwa na mikakati makini ya maendeleo, matumizi bora na sahihi ya rasilimali, kuunganisha nguvu, kwa kujikita katika kanuni ya auni kati ya mataifa; kuratibu na hatimaye, kupima maendeleo yaliyokwisha fikiwa.

Mikakati ya maendeleo ijielekeze zaidi kwa kuangalia uhalisia wa maisha ya watu husika kadiri ya mazingira yao; isikilize uzoefu wa watu husika na kutoa majibu muafaka kwa kusoma alama za nyakati bila mizengwe ya kisiasa ambayo wakati mwingine imekwamisha mchakato wa maendeleo endelevu miongoni mwa watu.

Ni mchango uliotolewa hivi karibuni na Askofu mkuu Bernadito Auza, Mwakilishi wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa katika mkutano wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa lililokuwa linajadili kuhusu maendeleo. Mikakati ya kupambana na umaskini ijielekeze zaidi katika sera zinazodumisha mshikamano, ushirikishwaji wa watu pamoja na kutoa fursa za ajira kwa watu kumudu gharama za maisha.

Pengo kati ya maskini na matajiri ni changamoto kubwa inayopaswa kufanyiwa kazi, ili kukuza na kudumisha amani na utulivu kati ya jamii, kwani kinzani na migogoro mingi kwa sasa ni matokeo ya kundi kubwa la maskini kuendelea kuogelea katika umaskini wa hali na kipato na watu wachache kuendelea kufaidika na rasilimali na utajiri wa nchi. Kutokana na hali kama hii, utu na heshima ya binadamu vinawekwa rehani. Wanawake washirikishwe katika kuibua, kupanga na kutekeleza mikakati ya maendeleo katika nchi zao na kwamba, huduma ya elimu, afya na maendeleo, itolewe bila ubaguzi.

Ujumbe wa Vatican katika mkutano huu, unapongeza nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa ambazo zimefanikiwa kupunguza tofauti za usawa wa kijinsia kwa kusema kwamba, bado kuna kazi kubwa inayopaswa kutendwa, ili kweli wanawake waweze kushirikishwa kikamilifu katika masuala yanayohusu mikakati ya maendeleo na maboresho ya maisha. Ikumbukwe kwamba, umaskini unaweza kujionesha katika medani mbali mbali za maisha na wala si tu kwa mtu kukosa fedha.

Mikakati ya maendeleo inapaswa kumlenga mtu mzima: kiroho na kimwili; kwa kuwekeza katika matumizi bora ya rasilimali na utajiri wa nchi, ili kusaidia mchakato wa kuleta maboresho ya maisha ya watu wengi zaidi. Lengo la Jumuiya ya Kimataifa katika kupambana na baa la umaskini awe ni binadamu na mahitaji yake msingi na wala si maendeleo ya vitu, huu ndio mshikamano wa kweli unaopaswa kuoneshwa na Jumuiya ya Kimataifa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.