Radio Vatican iliyoanzishwa kunako tarehe 12 Februari 1931, inaendelea kusoma alama
za nyakati, ili kwenda sanjari na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari, kwa
kuhakikisha kwamba, "inakula sahani moja na wasikilizaji, wasomaji na watazamaji wake"
kwa kutumia mitandao ya mawasiliano ya kijamii.
Ni Radio inayomilikiwa na
kuendeshwa na Vatican ambayo inapenda kujielekeza zaidi katika kuhabarisha walimwengu
kuhusu maisha na utume wa Baba Mtakatifu; mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaotekelezwa
na Mama Kanisa katika maisha ya watu: kiroho na kimwili; masuala ya Jumuiya ya Kimataifa;
majadiliano ya kidini na kiekumene; muziki na mambo mengi ambayo kimsingi ni sabuni
ya roho kwa wasikilizaji wengi!
Utajiri wote huu unapatikana katika lugha
arobaini zinazotumiwa na Radio Vatican kurusha matangazo yake sehemu mbali mbali za
dunia; Lugha ya Kiswahili, ikipewa kipaumbele cha pekee kwa Bara la Afrika. Katika
maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria wa Guadalupe, uongozi wa Radio vatican umezindua
mtandao mpya wa Radio Vatican unaojitahidi kusoma alama za nyakati katika mchakato
wa maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari, ili kuweza kuwafikia watu wengi zaidi,
huko walikojichimbia, lakini wana kiu ya kutaka kusikia kile kinachoendelea katika
maisha na utume wa Kanisa.
Mtandao mpya wa Radio Vatican ambao umefanyiwa maboresho
makubwa kwa sasa utapatikana katika lugha 37 kufuatana na mpangilio wa Alfabeti, lengo
ni kuiwezesha Radio Vatican kuendeleza mchakato wa majadiliano kwa kutumia mitandao
ya kijamii, utume unaotekelezwa kwa kushirikiana pia na Kituo cha Televisheni cha
Vatican kinachotoa picha za matukio makuu yanayofanywa na Baba Mtakatifu katika maisha
na utume wake.
Kwa njia ya teknolojia ya mawasiliano, watu kutoka sehemu mbali
mbali za dunia wanaweza kufuatilia matukio kwa lugha mbali mbali kutoka katika mtandao
wa Radio Vatican na kwa matukio makuu, Radio Vatican pia inaendesha programu za moja
kwa moja katika baadhi ya lugha. Takwimu zinaonesha kwamba, watumiaji wa mtandao wa
Radio Vatican wamegawanyika kama ifuatavyo:
Ulaya watumiaji wa mtandao wa
Radio Vatican ni asilimia 57% Bara la Amerika ni asilimia 29.14% Bara la Asia
na Oceania ni asilimia 11.22% Bara la Afrika ni asilimia 2.50%.
Watumiaji
wa mtandao wa Radio Vatican kwa kufuatia jinsia wamegawanyika kama ifuatavyo: Wanawake
ni asilimia 46% na wanaume ni asilimia 54%. Jambo la kufurahisha ni kuona kwamba,
watumiaji wengi wa mtandao wa Radio Vatican ni vijana wenye umri chini ya miaka 35.
Radio Vatican, mkongwe katika mawasiliano ya jamii, inaendelea kusoma alama za nyakati
kwa kuhakikisha kwamba, inatekeleza dhamana na wajibu wake mintarafu maendeleo ya
sayansi na teknolojia ya habari kwa watu wa kizazi kipya.
Lengo ni kuendeleza
mchakato wa mawasiliano na kuliwezesha Kanisa kukuza na kudumisha majadiliano katika
maisha na utume wake kwa njia ya matumizi ya mitandao ya kijamii!
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.