2014-12-11 10:06:19

Ukata unatisha Malawi!


Tume ya haki na amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi inasema kwa sasa Malawi inakabiliwa na ukata mkubwa kutokana na ukweli kwamba, wafadhili mbali mbali waliokuwa wanachangia katika bajeti ya Serikali wamejitoa kutokana na ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma. Tume ya haki na amani inasema, kwa hakika Malawi bado inahitaji kupata misaada kutoka kwa wafadhili, vinginevyo watu wengi wataendelea kuteseka sana.

Jambo la msingi ni wadau kwa kushirikiana na Serikali kuhakikisha kwamba, fedha inayotolewa inawafikia walengwa pamoja na kuwawajibisha kisheria watu waliokwapua mamillioni ya dolla za kimarekani kwa ajili ya mafao yao binafsi, ili wawe fundisho kwa watu wenye tabia chafu inayodidimiza mchakato wa maendeleo na mafao ya wengi nchini Malawi.

Katika miaka ya hivi karibuni ubora wa huduma ya afya, elimu na maji umeendelea kudidimia kwa kiasi kikubwa kiasi cha kuhatarisha usalama na maisha ya wananchi wa Malawi. Baadhi ya huduma zimeanza kutolewa na Makampuni ya watu binafsi, jambo ambalo si rahisi kwa wananchi wengi wa Malawi kuchangia katika huduma hizi. Wananchi wa Malawi wameanza kuwawajibisha viongozi na wafanyakazi wa umma wanaoonesha tabia ya wizi na ufisadi wa fedha na mali ya umma, kwani wamechoshwa kuona watu wakimezwa na uchu wa mali!







All the contents on this site are copyrighted ©.