2014-12-10 10:54:34

Mwongozo wa Sinodi ya Maaskofu 2015


Sekretarieti ya Sinodi za Maaskofu imechapisha Mwongozo wa Sinodi ya Kawaida ya Maaskofu itakayoadhimishwa mjini Vatican kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 25 Oktoba 2015, kwa kuongozwa na kauli mbiu "Wito na Utume wa Familia katika Kanisa na Ulimwengu mamboleo".

Mwongozo wa Kazi, unaojulikana katika lugha ya Kilatini kama "Lineamenta" ni hati ya kwanza kutolewa katika mchakato wa maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu na kwa namna ya pekee, kama ilivyoelekezwa na Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kufunga rasmi maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu, iliyoadhimishwa mjini Vatican, mwezi Oktoba 2014. Mwongozo huu unatokana na Hati ya Mababa wa Sinodi, "Relatio synodi" iliyotolewa wakati wa maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu na kwa sasa imewekwa katika mfumo wa maswali, ili kusaidia mchakato wa maandalizi ya hati ya pili, ijulikanayo kama Hati ya Kutendea Kazi, "Instrumentum Laboris.

Hati hii imetumwa kwa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki sehemu mbali mbali za dunia, kwa wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume na kwa Sekretarieti ya Vatican. Lengo la Hati hii kuiwezesha Familia ya Mungu kuanza kuchangia kwa kina na mapana hoja mbali mbali zitakazofanyiwa kazi na Mababa wa Sinodi kuhusu familia.

Matunda ya kazi hii yatakusanywa na Sekretarieti ya Sinodi za Maaskofu ili kuandaa Hati ya Kutendea Kazi, "Instrumetum Laboris". Ili kufanikisha zoezi hili, majibu kutoka kwenye Mabaraza ya Maaskofu na wadau mbali mbali hayana budi kuwa yameifikia Sekretarieti ya Sinodi za Maaskofu ifikapo tarehe 15 Aprili 2015, tayari kuendelea na hatua nyingine zaidi.

Waamini wanaalikwa kwa mna ya pekee, kuendelea kuwasindikiza Mababa wa Sinodi kwa njia ya sala na maadhimisho mbali mbali yanayopania kutangaza Injili ya Familia kati ya Watu wa Mataifa. Sherehe ya Familia Takatifu kwa Mwaka 2014 ipewe kipaumbele cha pekee na wanafamilia wote, ili kuonesha umoja, upendo na mshikamano katika wito na maisha ya kifamilia.







All the contents on this site are copyrighted ©.