2014-12-10 12:03:58

Damu ya watu wasiokuwa na hatia inawalilieni!


Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati katika mahubiri yake wakati wa maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, iliyofanyika tarehe 8 Desemba 2014, amewataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini humo kutubu na kumwongokea Mungu, ili kuanza kujikita katika mchakato wa msamaha na upatanisho wa kitaifa kwa kuachana na matendo ambayo yanagumisha ustawi na maendeleo ya watu!

Umefika wakati wa kuachana na mapambano ya silaha ambayo yamekuwa ni janga la kitaifa tangu nchi hii ilipojitwalia uhuru wake, kwa matajiri kuwatumia wanyonge kwa ajili ya mafao yao binafsi, huku wakiwaacha katika mateso na hali ya kukata tamaa. Umefika wakati wa kutubu na kujipatanisha na nafsi pamoja na jamii inayowazunguka ili kuanza mchakato wa upatanisho wa kitaifa. Watu wajenge tabia ya kusema na kusimamia ukweli unaowaweka huru badala ya kuendekeza majungu na umbea ambao kamwe si mtaji, kama ni hivi anasema Askofu mkuu Nzapailanga, wengi wangekwisha kutajirika.

Waamini na wananchi wa Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati wanapaswa kujielekeza zaidi katika mchakato wa: haki, amani, msamaha na upatanisho, ili kuwaelekeza watu katika njia inayowaongoza katika maendeleo endelevu badala ya kuendelea kuogelea katika vita na maafa kwa watu na mali zao. Watu wanahitaji maendeleo na wala si vita na kinzani.

Askofu mkuu Nzapalainga anawataka wafanyabiashara wanaoendelea kujitajirisha kwa kuuza silaha, wakumbuke kwamba, damu ya watu wasiokuwa na hatia inawalilia. Hii ni changamoto hata kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, inadhibiti biashara ya silaha kimataifa ili kupunguza vita, migogoro na kinzani zinazoendelea kuwa ni chanzo kikuu cha maafa na umaskini. Umefika wakati kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kukimbilia neema, huruma na upendo kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa njia ya toba, msamaha na upatanisho wa kweli unaotoka katika undani wa mtu, ili kwa pamoja, wananchi wote kutoka Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, waweze kutembea katika njia ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa!







All the contents on this site are copyrighted ©.