2014-12-09 15:45:16

Ziara ya Kardinali Leonardi Sandri nchini Ethiopia.


Kardinali Leonardi Sandri, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki, yuko ziarani Ethiopia, kama mjumbe wa Papa katika maadhimisho ya kutimia miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Ethiopia. Kati ya mambo mengine, hotuba zake amekazia umuhimu wa kuwa na umoja kwa wafuasi wa Kristo , kuunda Kanisa Moja Takatifu na la mitume.

Katika ziara hii aliyoianza Ijumaa tarehe 5 Desemba, siku ya Jumamosi 6 Desemba, alishiriki Ibada ya Misa iliyosomwa kwa kufuata maadhimisho ya Liturujia Kanisa la Alesandria la Ethiopia , iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Gheez, mjini Addis Ababa, Ibada iliyohudhuriwa pia na Nunsio wa Papa Ethiopia,Askofu Mkuu Luigi Bianco, pamoja na Askofu Mkuu wa Addis Ababa, Askofu Mkuu Berhaneiesus Souraphiel, na Maaskofu wengine , kutoka nchi za Mashariki ya Kati.

Baada ya Misa, Kardinali alitoa kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francis, Baraka ya Kichungaji, na kukabidhi kwa Askofu Mkuu wa Addis Ababa, medali ya mwaka wa pili wa utawala wa Kipapa wa Papa Francisko.

Na baadaye Kardinali Sandri, akifuatana na Nunsio na Askofu Mkuu Mousie wa Upatriaki wa Mashariki mwa Ethiopia , walikutana na watu mbalimbali katika maeneo waliyo yatembelea ikiwemo Hospitali ya Mtakatifu Luke, inayomilikiwa na Baraza la Maaskofu wa Ethiopia, ambako Kardinali Sandri alitoa salaam za Papa na mchango wa taasisi kadhaa, hasa kutoka Baraza la Maaskofu Italia, na pia shukrani kwa namna ya kipekee kwa Shirika la Masista la Tamil Nadu (India) na madaktari wa CUAMM wa Verona Italia, kwa huduma yao katika hospitali hiyo.

Aidha Kardinali alikutana na vijana na Maskauti katika Parokia moja wakiwa na mchungaji wao, ambako aliweza kusikiliza historia na shughuli za Taasisi, ambayo ni pamoja shule uuguzi, ambako kuna vijana walio mafunzoni wapatao 600. Taasisi ambayo kwa sasa ina umri wa miaka 14 tangu kuanzishwa.

Kwa siku ya Jumatatu, Kardinali pamoja na mambo mengine ,alikwenda katika Seminari Kuu ambako aliweza kufanya majadiliano na waseminaristi , Mapadre na Masista na wafanyakazi katika maeneo mbalimbali. Kati ya maswali aliyoulizwa yalilenga zaidi katika ukweli wa kiekumeni na mazungumzo kati ya nchini Ethiopia hasa katika mtazamo kwamba hivi karibuni pia alipata nafasi ya kuandamana na Papa Francisko, katika ziara ya kitume huko Uturuki. Nchi hizi mbili, Uturuki na Ethiopia zote zina idadi ndogo ya Wakatoliki wanaoisha kati ya idadi kubwa ya waumini wa Kiislam . Na pia maswali mengine yalilenga katika kutafakari uhusiano kati ya ethiopia na Eritrea, ambamo katika ngazi ya Kanisa, ni familia moja kubwa ya kanisa la Alesanderia yenye kufuata liturujia ya gheez.Lakini tofauti za kisiasa kwa mataifa haya mawili, zinafanya watu wanaishi kwa shida kubwa, kutokana na mtafaruko huo. Kardinali katika majibu yake, ametoa wito kwa raia wa nchi hizi mbili , kutafakari kwa kina nini maana ya kusihi kwa amani na utulivu, na warejee katika maridhiano na amani.

Kardinali aliikamilisha siku ya Jumatatu kwa kushiriki adhimisho la Ekaristi kwa ajili ya Siku Kuu ya Maria Mkingiwa dhambi ya asili.








All the contents on this site are copyrighted ©.