Ungeni mkono mchakato wa kupambana na utumwa mamboleo!
Baraza la Makanisa Ulimwenguni linawapongeza viongozi wa kidini waliotia sahihi tamko
la pamoja linalowawajibisha kimaadili kupambana kwa nguvu zote dhidi ya utumwa mamboleo
unaojionesha kwa namna ya pekee katika biashara haramu ya binadamu, tamko ambalo limetolewa
hivi karibuni mjini Vatican.
Baraza la Makanisa Ulimwenguni linasema kwamba,
kila mwanadamu ameumbwa huru na Mwenyezi Mungu; jambo ambalo linapaswa kuendelezwa
kwa kujenga na kudumisha mafao ya wengi, usawa na udugu kati ya watu. Utumwa mamboleo
unaofumbatwa katika biashara haramu ya binadamu, kazi za suluba, ukahaba, biashara
ya viungo vya binadamu, ndoa shuruti pamoja na mambo yote yasiyoheshimu na kuthamini
utu na heshima ya binadamu, hayana budi kuchukuliwa kuwa ni uhalifu dhidi ya ubinadamu.
Dr.
Fulata Mbano-Moyo mjumbe kutoka Baraza ya Makanisa Ulimwenguni aliyehudhuria katika
tukio hili anasema kwamba, utumwa mamboleo unawageuza watu ambao wameumbwa kwa sura
na mfano wa Mungu kuwa ni bidhaa zinazokidhi tamaa za kimwili na nguvu kazi inayohitajika
katika mchakato wa uzalishaji mali. Baraza la Makanisa ni kati ya wadau wakuu wanaotaka
kuona kwamba, utumwa mamboleo unatoweka katika uso wa nchi.
Kwa miaka mingi
kumekuwepo na mapambano dhidi ya utumwa mamboleo pamoja na watu kudai haki zao msingi
kwa kupinga vitendo vya ubaguzi wa rangi na jinsia; mambo ambayo yanawanyanyasa utu
na heshima ya binadamu. Changamoto kubwa iliyoko kwa wakuu wa dini mbali mbali duniani
ni kuhakikisha kwamba, tamko hili linavaliwa njuga ili liweze kutekelezwa katika ngazi
mbali mbali.
Tukio la kuutia sahihi kwa Tamko hili lilihudhuriwa na viongozi
wanawake kadhaa, changamoto ya kuhakikisha kwamba, kweli utumwa mamboleo unafutika
kutoka katika uso wa dunia kwa kuwa waathirika wakubwa zaidi ni wanawake na watoto.
Makanisa wanachama ambayo bado hayaweka sahihi katika Tamko hili yanahimizwa kufanya
hivyo mapema iwezekanavyo.
Baba Mtakatifu Francisko katika tukio hili alisema
kwamba, Tamko hili ni tukio la kihistoria, linalowahamasisha wakuu wa dini kuchukua
hatua madhubuti katika mapambano dhidi ya utumwa mamboleo ambao leo ni hii ni janga
na uhalifu dhidi ya ubinadamu. Ni janga linalogusa maisha ya watu: kiuchumi, kijinsia,
kisaikolojia pamoja na kudhalilisha wahanga wa vitendo hivi vya kinyama.
Mtandao
Mpya wa Uhuru Duniani unapania pamoja na mambo mengine kuhakikisha kwamba, utumwa
mamboleo unakomeshwa kwa kung'oa mizizi, ili Jamii iweze kuwa ni mashahidi wa huruma
ya Mungu na upendo kwa watu wote waliotumbukizwa katika utumwa mamboleo. Takwimu zinaonesha
kwamba, kuna watu zaidi ya millioni ishirini nukta tisa wametumbukizwa katika kazi
za suluba sehemu mbali mbali za dunia. Hawa ni watu wanaouzwa kama bidhaa katika soko
la biashara haramu ya binadamu au wametumbukizwa katika biashara ya ngono.