Vatican inaendelea kukazia sera za ukweli, uwazi na uwajibikaji katika masuala ya
fedha za Kanisa
Kardinali George Pell, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uchumi katika mahojiano maalum
na Gazeti la Herald anasema kwamba, hali ya fedha mjini Vatican ni nzuri kuliko ilivyokuwa
inafikirika, kwani kuna kiasi kikubwa cha Euro kilichokuwa hakikuoneshwa kwenye Bajeti
ya Vatican, lakini mchakato wa mabadiliko na muundo mpya wa fedha mjini Vatican unaokazia:
ukweli, uwazi, kanuni na sheria za kimataifa kuhusu fedha unaanza kuonesha mafanikio
makubwa.
Lengo ni kuhakikisha kwamba, fedha ya Kanisa inatumika vizuri kwa
ajili ya kusaidia mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima:
kiroho na kimwili. Kardinali Pell anasema, miaka kadhaa iliyopita kulikuwa na usiri
mkubwa kuhusu fedha hali ambayo ilikuwa ni hatari sana kwani ingeweza kulitumbukiza
Kanisa katika kashfa ya utakatishaji wa fedha haramu.
Kashfa ya kuvuja kwa
nyaraka za siri mjini Vatican ni mambo yaliyoacha uchungu mkubwa katika maisha na
utume wa Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI. Mchakato wa mabadiliko ulioanzishwa
na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican unaendelea kuonesha mafanikio makubwa kwa
kuwa na udhibiti wa mali na fedha ya Kanisa, dhidi ya wajanja wachache wanaotaka kujitajirisha
wenyewe.
Akizungumzia kuhusu taarifa hii, Padre Federico Lombardi Msemaji mkuu
wa Vatican anafafanua kwamba, fedha inayotajwa si fedha haramu, bali ni fedha ambayo
haikuwa imeoneshwa kwenye bajeti ya Vatican na kwamba, hiki ni kielelezo makini cha
ushirikiano mkubwa zaidi wa taasisi mbali mbali katika udhibiti wa fedha ya Kanisa.
Ikumbukwe kwamba, taarifa ya Bajeti ya Vatican iliyokuwa inapitishwa kila mwaka na
Baraza la Makardinali kumi na watano, iligusa baadhi ya taasisi kubwa za Vatican na
wala si vatican yote.
Padre Federico Lombardi pia anasema, kuna watu wawili
waliokuwa wanafanya kazi kwenye Benki ya Vatican, IOR, wamefikishwa mahakamani kufuatia
tuhuma za kujihusisha na kufanya manunuzi kinyume cha sheria kati ya mwaka 2001 hadi
mwaka 2008 na kwamba, akaunti zao za Benki zimefungwa.