Kwa waamini wanaojongea kupokea Sakramenti ya Upatanisho, wanaonja huruma Mungu na
kuondolewa dhambi zao sanjari na kupatanishwa na Kanisa ambalo limejeruhiwa kutokana
na dhambi zinazotendwa na watoto wake, lakini kwa njia ya mapendo, mfano na sala linashughulikia
kwa bidii wongofu wa watoto wake. Wongofu ni hatua ya kwanza kwa mwamini kuweza kumrudia
tena Yesu, kwa kufanya toba na kutumiza malipizi ya dhambi.
Maaskofu
na Mapadre ndio wahudumu wa Sakramenti ya Upatanisho na wenye uwezo wa kusamehe dhambi
kwa njia ya Fumbo la Utatu Mtakatifu. Padre anapoadhimisha Sakramenti ya Kitubio anatekeleza
dhamana na huduma ya mchungaji mwema, anayetafuta Kondoo aliyepotea; huduma ya Msamaria
mwema anayeponya majeraha; huduma ya Baba mwenye huruma anayemngoja Mwana mpotevu
aweze kurejea tena nyumbani. Hii ni huduma ya hakimu mwenye haki, huruma na mapendo.
Kimsingi, Padre ni chombo cha huruma na mapendo ya Mungu kwa wakosefu.
Kwa
kutambua umuhimu wa Sakramenti ya Upatanisho katika maisha na utume wa Kanisa, Idara
ya Toba ya Kitume, hivi karibuni imeandaa kongamano ambalo limewashirikisha watu mbali
mbali, ili kuchambua kwa pamoja umuhimu wa kulinda na kutunza siri ya maungano; ambayo
kwa mtu anayebainika kwamba, ameivunja anatengwa na Kanisa, kadri ya Sheria za Kanisa.
Hapa wanahusika hata wale wanaotumia njia za mawasiliano ya kisasa ili kusambaza siri
za maungano.
Kardinali Mauro Piacenza, Mkuu wa Idara ya Toba ya Kitume anasema
kwamba, siri ya maungano inakwenda sambamba na Sakramenti ya Daraja Takatifu na kwamba,
wahudumu wa Sakramenti hii, hawana sababu wala kuruhisiwa kutoa kwa mtu yoyote yule
siri za maungamo; lengo ni kuhakikisha kwamba, Mama Kanisa anatunza kwa heshima na
upendo mkuu mahusiano ya ndani kabisa kati ya Mwenyezi Mungu na mwamini anayetubu
dhambi zake. Kanisa linapania kulinda heshima ya mwamini na haki zake msingi.
Monsinyo
Krzysztof Nykiel, Afisa katika Idara ya Toba ya Kitume anasema, Mama Kanisa kwa wakati
wote wa historia yake, ametoa kipaumbele cha kwanza kwa ajili ya Sakramenti ya Upatanisho;
mahali ambapo mwamini anapata fursa ya kukutana ana kwa ana na Padre kwa ajili ya
maungamo; dhamana inayojikita katika kanuni maadili, sheria za Kanisa na ufafanuzi
wa kitaalimungu, kama ilivyofafanuliwa kwa kina na mapana wakati wa Maadhimisho ya
Mtaguso mkuu wa Laterano uliofanyika kunako mwaka 1215 kwa kuweka sheria na adhabu
kwa Wakleri watakaovunja siri ya maungamo.
Monsinyo Nykiel anasema, siri ya
maungamo inawafunga hata watu wale ambao kwa bahati mbaya wameweza kusikia maungano
kati ya mwamini na Padre; kwani hapa kinachosisitiziwa ni mahusiano kati ya muungamaji
na Mwenyezi Mungu. Maungamo hayana budi kufanyika kwa kusikiliza kwa siri na wala
si kutangaza hadharani, ndiyo maana Mama Kanisa anakazia utakatifu wa siri ya maungamo
ambayo haiwezi kutolewa hadharani hata kama itampasa Padre kuyamimina maisha yake.
Wawezeshaji wakati wa kongamano hili wamekazia pamoja na mambo mengine umuhimu
wa mawasiliano kati ya watu hasa wakati huu wa maendeleo ya sayansi na teknolojia
ambayo inawezesha mwanadamu kuwa na mwingiliano mkubwa , hali ambayo wakati mwingine
inamfanya mtu kuwa ni tegemezi. Wajumbe wamefahamishwa pia kuhusu siri ya maungamo
mintarafu mwelekeo wa kifalsafa na kitaalimungu, kwa kukazia ukweli dhidi ya uongo;
mahusiano ya dhati kati ya Kanisa kama taasisi na ukuu wa Mungu.
Kardinali
Mauro Piacenza amekumbusha kwamba, maungamo yanamsaidia mwamini kupunguza mzigo wa
dhambi, kwa kuonjeshwa huruma na upendo wa Mungu unayojionesha kwa namna ya pekee
katika moyo wa toba na unyenyekevu. Baada ya mwamini kuondolewa dhambi zake, Mwenyezi
Mungu mwingi wa huruma na mapendo, hakumbuki tena dhambi zilizotendwa na mwamini,
kwani zimesamehewa kutokana na ukuu wa Mungu.
Wawezeshaji wamekazia pia umuhimu
wa kupokea Sakramenti ya Upatanisho pamoja na mwamini kuendelea kusindikizwa katika
hija ya maisha yake ya kiroho, ili aweze kufundwa zaidi kutoka katika undani wake.
Kuna mwelekeo mkubwa kwa sasa vijana kutaka kusikilizwa kwa makini zaidi; kwa kujenga
na kudumisha mahusiano yanayojikita katika ukweli, huruma na katika maelekeo ya kuweza
kujipatia wokovu.
Kardinali Mauro Piacenza anasema haki ni njia nyingine ambayo
inaonesha jinsi ambavyo Mwenyezi Mungu anampenda mwanadamu na kumtakia mema. Mwenyezi
Mungu anatumia haki ili kupenda na kwamba, haki ni chemchemi ya mapendo yanayobubujika
kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya
Kiswahili ya Radio Vatican.