2014-12-06 10:51:09

Sherehe ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili


Kardinali Agostino Vallini, Makamu Askofu Jimbo kuu la Roma anapenda kuwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuungana na Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 8 Desemba.

Maadhimisho haya yatafunguliwa kwa Kikosi cha zimamoto kuweka shada la maua katika Sanamu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, iliyopo kwenye Uwanja wa Spagna, kama kumbu kumbu endelevu iliyofanywa na Kikosi cha Zima moto tarehe 8 Desemba 1857. Baba Mtakatifu anatarajiwa kuwasili kwenye Uwanja wa Spagna majira ya saa 10: 00 jioni na kulakiwa na viongozi wa Kanisa na Serikali.

Kardinali Vallini anasema, kutakuwepo na umati mkubwa wa wagonjwa watakaosindikizwa na Chama cha Kitaifa cha Kuwahudumia Wagonjwa, UNITALSI, ili kutoa heshima yao kwa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili pamoja na kusalimiana na Baba Mtakatifu Francisko ambaye katika maisha na utume wake, anaendelea kuwapatia wagonjwa na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kipaumbele cha kwanza. Kimsingi, Sherehe ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili inapania kuwa ni siku ya sala, tafakari na mshikamano na maskini.







All the contents on this site are copyrighted ©.