Niliwahi kumsikia dada mmoja akimwita mdogo wake Imakulata kwa ufupisho: “Makulataaa!
Unaitwa na mama!” Jina Makulata jinsi alivyolitumia dada huyu linatokana na neno la
kilatini “makula” maana yake ni doa au uchafu. Kinyume chake ni Imakulata, maana yake
kutokuwa na doa au uchafu wala takataka yoyote ile.
Leo kanisa
katoliki popote duniani linasherehekea sikukuu ya Bikira Maria Imakulata, yaani Maria
msafi mbele ya Mungu, asiye na dhambi kwani alikingwa tangu kuzaliwa kwake. Katika
kanisa fundisho hilo la Maria kuwa Immakulata linaitwa Dogma. Dogma hiyo ilitangazwa
rasmi tarehe nane Desemba mwaka 1854 na Baba Mtakatifu Pius wa tisa. Toka hapo katika
nchi nyingi duniani, kanisa katoliki limemchagua Imakulata kuwa mlinzi wa Taifa lao.
Kadhalika katika Afrika, kuna nchi nyingi, kama vile Jamhuri ya Congo na Jamhuri
ya Muungano ya Tanzania wamemchagua Maria Imakulata kuwa mlinzi wa Taifa. Kwa nchi
ya Tanzania sikukuu hiyo imepangwa siku moja kabla ya sikukuu ya kupata uhuru wake
wa kisiasa toka kwa wakoloni. Dogma ni lugha tata isiyoeleweka kirahisi na mtu wa
kizazi cha leo. Lakini yabidi ieleweke kuwa Dogma yoyote ile ni tamko la kibinadamu
siyo amri ya Mungu.
Tamko hilo linatafsiri ukweli wa Neno la Mungu lililo
katika Biblia. Kwa vyovyote, lugha hii ya kibinadamu ambayo ni Dogma inategemea sana
mabadiliko ya hali halisi ya maisha ya jamii. Kwa hiyo dogma ni tafsiri ya maisha
mbayo inabidi irandane na ukweli wa maisha. Dogma ya Bikira Maria Imakulata mkingiwa
dhambi ya asili imewekwa hivi kwamba iweze kuigusa jamii yetu ya leo. Kwa maana hiyo,
yaonekana hali ya maisha na matendo ya Mama huyu Maria yanalingana na hali halisi
ya mazingira yetu ya sasa.
Ukweli huo hauna upinzani, kwani Maria alikuwa
mtu kama sisi, alizaliwa kama watu wengine huko Galilea, alipokuwa msichana akampenda
kijana Yosefu, na akategemea kuolewa naye wakiwa na malengo ya kupata watoto na kuijenga
familia yao kadiri ya mila na desturi za utamaduni wa waana wa Ibrahimu. Akiwa sawa
kama watu wengine, mama huyu alipambana pia na makashkash ya maisha, na alishawishiwa,
kwani hata mwanae Yesu alishawishiwa pia. Tofauti ya Maria na watu wengine ni hii
kwamba Mungu aliona katika Maria utayari kamili uliomvuta amchague kumtumia katika
mradi wake wa kuukomboa ulimwengu.
Hebu tuiangalie sikukuu yetu katika mwanga
wa somo la kwanza la leo ili tuweze kuelewa na kufaidika na dogma ya Imakulata. Fasuli
hii inahusu kuanguka kwa Adamu na Eva katika dhambi. Habari hii imeundwa kadiri ya
mantiki ya kifilosofia na teolojia ya wakati huo, na ni lugha ngumu kueleweka kwa
watu wa sasa. Ukweli uliojulikana enzi hizo hadi leo kuwa sisi binadamu tumeathirika
na dhambi ya asili aliyoitenda Adamu na mke wake Eva.
Hapo haieleweki ni kwa
hoja ipi adhabu hiyo tupewe sisi tusiohusika na kosa walilolitenda wazee hawa. Ukweli
ni kwamba habari hiyo isichukuliwe kuwa kama simulizi la kihistoria ya maovu yalivyotendwa
na Adamu na Eva.
Fasuli hii inataka kutoa fundisho la kiteolojia linalojibu
kwa lugha ya kimistiki (myth) maovu na utata wa maisha anaokumbana nao binadamu. Hasahasa
inalenga kujibu swali la kwa nini kuna uovu, uharibifu, na ukosekanaji wa haki hata
mauaji hapa duniani. Ukweli ni kwamba binadamu mwenyewe yaani wewe na mimi ndiyo Adamu
na Eva. Ni sisi ndiyo tulio kinyume na mwito aliotuitia Mungu wa jinsi njema ya kuishi
hapa duniani. Kutokana na ukweli huo, hata dogma ya Imakulata inadai kuitazama kwa
kina na kuielewa kwa namna mpya.
Tuangalie kinaganaga maelezo na ujumbe wa
anguko la wazee wetu wa kwanza. Mungu aliumba ulimwengu kwa muda wa siku saba, namba
inayoonesha ukamilifu. Halafu inarudiwa kusemwa mara nyingi kuwa, baada ya uumbaji
akaona kila kitu alichokiumba kuwa ni chema. Maana yake kulikuwa na amani, ushirikiano,
wema kati ya Mungu na binadamu. Binadamu aliishi vyema na kwa amani hata kati ya bwana
na bibi. Kila mmoja alijisikia kuwa ni zawadi kwa mwingine.
Katika mazingira
mazuri kama hayo anajipenyeza nyoka. Huyo anafika na kushawishi kuvunja mahusiano
hayo mazuri. Anamshawishi binadamu kumpindua Mungu, ili abaki mwenyewe wa kupanga
na kuamua mambo yake. Hadithi za nyoka na shetani zinatokana na marabi wa kiyahudi
waliokuwa wameathirika na mithi za mila za Wapersia.
Hao ndiyo walioanza
kumwona shetani katika umbo la nyoka kuwa kama mpinzani au kinyume cha Mungu. Nyoka
au shetani anaoneshwa kuwa ni mwerevu, mwongo na mjanja sana. Ujanja au werevu ambao
ni udanganyifu wa kutaka kurubuni hekima ya Mungu na mapato yake unaishia kujirubuni
wenyewe na kuvunjisha mahusiano na Mungu na ya wengine.
Mungu anamwita Adamu
na kumwuliza “Uko wapi”. Ni tofauti na kuuliza “Upo wapi” yenye maana ya pahala. Bali
aliuliza “Uko wapi?” akimaanisha anajisikiaje, ana hali gani hasa baada ya kujitenga
na Mungu.
Sikiliza majibu ya Adamu na linganisha na kitokeacho katika historia
ya binadamu. “Niliogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha.” Kwa hiyo pato la kwanza
la kukata mawasiliano na Mungu ni kuwa mtupu bila kitu, kisha unajionea aibu mwenyewe.
Angalia
pia leo ulimwengu wa watu waliomwacha Mungu na kufuata vichwa vyao jinsi wanavyoishi.
Yote yanatokana na kujiweka sisi kwanza badala ya kumweka Mungu kwanza. Adamu anapodadisiwa
zaidi anajietea, “ni mwanamke uliyenipa”. Kwa hiyo pato jingine la kuvunja mawasiliano
na Mungu ni kuvunja mahusiano na wenzako.
Binadamu anamlaumu mke wake, ambaye
Mungu amemweka kando yake. Mbaya zaidi, kosa linamrudia Mungu mwenyewe, analaumiwa
jinsi alivyomuumba vibaya. Amemtengeneza mwanamke mwenye roho mbaya. Mwanamke naye
anapita mulemule alimopita bwana wake. Anamlaumu nyoka.
Kwa namna fulani hata
Eva naye anamlaumu Mungu kwa kuumba mambo vibaya. Kwa hiyo wazee hawa wote wawili
kwa pamoja wanamlaumu Mungu kwa kuuumba vibaya ulimwengu huu. Mungu amekosea sana
kuweka ndani mwetu uhalisia wa wema na ubaya. Ametuumba watu wenye mipaka ndiyo maana
hatupo tu wema moja kwa moja, bali kuna nguvu ya kugoma kufanya hata mambo yake Mungu
mwenyewe. Kwa hiyo Mungu mwenyewe amejipalia mkaa kichwa na ametujengea kiburi.
Hata
hivyo swali linalozidi kutukereketa linabaki: Je huyo nyoka atakuwa ndani yetu hadi
lini, yaani, uovu huo hauwezi kushindwa? Jibu la swali hilo linapatikana katika sikukuu
ya leo. Habari njema ya sikukuu ya leo, imeanza hapa unapoona wazi kabisa jinsi shetani
anavyoshindwa. Unamwona nyoka huyo hafiki mbali, kwani “Njia ya mwongo ni fupi, au
“ndege mjanja hunaswa kwenye tundu bovu”. Hapa unaona wazi kwamba baada ya kuhojiana
na Eva, Mungu hapotezi muda wake kumhoji nyoka, kwa sababu nyoka au ujanja na wongo
huo ni sehemu ya binadamu.
Basi ujanja na wongo huo unaambulia kupata hukumu
kali pale nyoka anapoambiwa: “Umelaniwa wewe kuliko hayawani wote walioko mwituni”.
Kulaaniwa maana yake kutokuwa na uzao yaani ni kufa na kufifia kabisa. Kisha anaambiwa
tena “utatambaa ardhini na kula mavumbi siku zote za maisha yako.”
Kwenda kwa
tumbo hakumaanishi kwamba kabla yake nyoka huyu alikuwa na miguu na alitembea la hasha,
bali ni lugha ya picha, kwamba sasa nyoka atagaagaa ardhini kama askari aliyeshindwa
na kujeruhiwa anavyojigalagaza ardhini mbele ya shujaa aliyemteka. Maana yake nyoka
atashindwa na kugaagaa chini baada ya kukatwa kichwa.
Hii ndiyo maana nzuri
ya sikukuu ya leo. Kwamba shetani atashindwa. Toka hapa kila mmoja wetu katika maisha
yake, ya imani, ya uongozi, ya kisiasa nk anaweza kuanza kufanya fikara zake. Kwamba
sisi kumbe ni akina Adamu na Eva na tumepagawa na nyoka mwerefu, mwongo, mjanja, mdanganyifu.
Tunaalikwa kumwangalia Maria jinsi alivyoishi maisha yake yote akiwa na umoja
na amani na Mungu. Hata kama katika Maria kulikuwa na huyo nyoka mwerevu, mjanja na
mwongo, aliyemjaribu kumwepusha na mawazo na fikra za Mungu, lakini shetani huyo hakufanikiwa
kumrubuni na kumwangusha.
Maria alikuwa daima mwaminifu kwa Mungu. Mama huyu
pekee ni alama ya ushindi wa Mungu dhidi ya uovu wa ulimwengu. Ndiyo maana anaitwa
Bikira Maria Immakulata. Sisi sote tumeitwa kuwa Imakulata. Tusikubali kuitwa “Makulataaa!”