2014-12-06 10:48:17

Kimbembe cha Uchaguzi mdogo Zambia!


Tume ya uchaguzi nchini Zambia imetangaza kwamba, wananchi wa Zambia watafanya uchaguzi mdogo hapo tarehe 20 Januari 2015 kufuatia kifo cha Rais Michael Chilufya Satta, kilichotokea hivi karibuni nchini Uingereza. Kinzani na mipasuko ya kisiasa inayoendelea kujionesha katika vyama vya kisiasa nchini Zambia haitazuia uchaguzi mdogo kufanyika kama ilivyopangwa.

Kutokana na changamoto hizi ambazo zinatishia usalama, amani na utulivu wa wananchi wa Zambia, Jukwaa la Wakristo nchini Zambia limeunda Kikosi kazi "CCMG" kitakachosimamia mchakato wa uchaguzi mkuu na hasa katika zoezi la kuhesabu kura, ambalo mara nyingi limekuwa ni chanzo cha vurugu na kutoweka kwa amani. Lengo ni kutaka kudumisha misingi ya haki, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa, ili kweli mchakato wa demokrasia uweze kushika mkondo wake na hatimaye, kuwapatia wananchi wa Zambia kiongozi atakayewaongoza ili kujiletea maendeleo endelevu.

Kikosi kazi katika waraka wake kwa wananchi wa Zambia kinasema, kinapenda kukazia na kudumisha misingi ya ukweli, uwazi na uhuru katika mchakato mzima wa uchaguzi mdogo nchini Zambia. Ili zoezi hili liweze kufanikiwa kuna haja kwa vyama vya kisiasa nchini Zambia kuchagua kiongozi bora atakayepimana nguvu na wengine, ili hatimaye, Zambia iweze kumpata Rais mpya.

Wananchi wote hawana budi kupania kujenga na kudumisha amani na utulivu wakati wote wa kampeni, lakini zaidi siku ya kupiga kura, ili kutoa nafasi kwa wananchi kutumia haki yao ya kikatiba kuchagua kiongozi anayewafaa. Ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba, inaunda mazingira yatakayowezesha uchaguzi kuwa huru na wa kweli sanjari na kudhibiti rasilimali fedha na watu, ili yote haya yatumike kwa ajili ya mafao, ustawi na maendeleo ya wananchi wote wa Zambia. Waandishi wa habari watekeleze dhamana na utume wao kwa kuzingatia kanuni maadili, weledi na sheria za nchi. Wanasiasa waepuke kampeni zinazojenga chuki, uhasama na ukabila kati ya watu.

Vijana wasikubali kutumiwa na wanasiasa uchwara ili kuvuruga amani na utulivu nchini Zambia, bali wahakikishe kwamba, viongozi watakaowachagua ni wale wanaopania kuwapatia fursa za ajira pamoja na kudumisha amani na utulivu nchini Zambia. Viongozi wa kijadi waheshimu utashi wa wananchi wa Zambia na uhuru wao wa kikatiba ili waweze kushiriki katika mchakato mzima wa uchaguzi mdogo. Viongozi wa kidini hawana budi kuachana na tabia ya kuwaalika baadhi ya wagombea Urais kutumia nyumba za Ibada kama majukwaa ya kisiasa, jambo linaloweza kuhatarisha amani na utulivu!

Vyama vya kiraia viwahamasishe wananchi wote kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mdogo na kwamba, Tume ya Uchaguzi nchini Zambia haina budi kuhakikisha kwamba, kweli uchaguzi unakuwa huru na wa haki; vyombo vya ulinzi na usalama vihakikishe kwamba, kuna amani na utulivu.







All the contents on this site are copyrighted ©.