Mchakato wa Uinjilishaji Barani Asia ni changamoto kwa Kanisa Barani Asia
Utume wa Kanisa Barani Asia ndiyo mada iliyochambuliwa hivi karibuni katika kongamano
la kimataifa lililoandaliwa na Shirika la Habari za Kanisa Barani Asia, “Asianews”
na kuadhimishwa kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbaniana. Baba Mtakatifu Francisko
katika ujumbe wake kwa washiriki wa kongamano hili, amewataka wahusika kuamsha tena
ari na shahuku ya kutaka kuzama zaidi katika mchakato wa Uinjilishaji Barani Asia.
Huu ni mwendelezo
wa changamoto ya Uinjilishaji inayotolewa na Mababa wa Kanisa katika mapambazuko ya
Millenia ya tatu ya Ukristo, utume ambao ulifunguliwa rasmi na Mtakatifu Yohane Paulo
II kunako mwaka 1995, na baadaye Baba Mtakatifu Francisko, mwezi Agosti, 2014 akafanya
hija yake ya kichungaji nchini Korea.
Baba Mtakatifu Francisko anaendelea
kulihamasisha Kanisa kutoka huko lilikojificha na kuwaendea watu wanaoishi pembezoni
mwa jamii kutokana na hali yao ya maisha, ili wao pia waweze kuonja huruma, upendo
na mshikamano unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa. Mwelekeo huu unajionesha katika
maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko ambaye mwanzoni mwa Mwaka 2015 anatarajiwa
kufanya hija ya kichungaji nchini Sri Lanka na Ufilippini, ili kuwaimarisha ndugu
zake katika Kristo kwa kuwaonjesha huruma na upendo na mshikamano kutoka kwa Kristo.
Kardinali
Luis Antonio Tagle, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Manila, Ufilippini anabainisha kwamba,
hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko nchini mwake, inaongozwa na kauli mbiu
ni “huruma na wema”, ili kuwagusa watu ambao wameathirika vibaya kutokana na tufani
ya, matetemeko ya ardhi; madhara ya rushwa na ufisadi wa fedha na mali ya umma; maskini,
watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.
Hija hii inapania kuamsha tena
dhamiri nyofu miongoni mwa wananchi wa Ufilippini. Ni huruma inayopaswa kutolewa pia
kwa maelfu ya wananchi wanaoishi kandoni mwa Bara la Asia. Ikumbukwe kwamba, Wakristo
Barani Asia wanaunda kundi dogo sana, ikilinganishwa na waamini wa dini nyingine;
hapa ni mahali ambapo Injili inatangazwa kwa njia ya mchakato wa majadiliano. Hija
ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Korea ya Kusini, iliwagusa wengi
na kuwaacha wameshikwa na bumbuwazi.
Wakristo wanaishi katika mazingira magumu
kutokana na baadhi ya waamini kuwa na misimamo mikali ya kiimani, inayogumisha misingi
ya haki, amani na utulivu. Kuibuka kwa kasi kubwa kwa vitendo vya kigaidi kunatishia
amani na usalama huko Mashariki ya Kati anasema Patriaki Louis Raphael Sako kutoka
Baghdad. Baba Mtakatifu Francisko anapotembelea katika maeneo kama haya, anakuwa kweli
ni faraja na changamoto ya matumaini kwa Wakristo wanaoteseka na kunyanyasika kutokana
na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Si rahisi kwamba, Wakristo waliokimbia makazi
yao wanaweza kurejea mapema hivi, bali itawachukua siku kadhaa hadi hali iweze kurejea
tena kama ilivyokuwa, ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa itashikamana kupinga biashara
ya silaha pamoja na kusitisha ufadhili kwa vikundi vya kigaidi vinavyoendelea kupandikiza
mbegu ya chuki na maafa kwa watu wasiokuwa na hatia.
Mtakatifu Yohane Paulo
II aliwahi kusema kwamba, Uinjilishaji Barani Asia ni changamoto kubwa kwa Kanisa
katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, changamoto ambayo kwa sasa inavaliwa
njuga na Baba Mtakatifu Francisko kwa kuanza kutembelea nchi kadhaa za Bara la Asia.
Ikumbukwe kwamba, kila siku ni siku ya Bwana, ni matumaini ya Kanisa Barani Asia kwamba,
Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai ataweza kubariki juhudi hizi za kimissionari
Barani Asia katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.