Mhariri wa Jarida "La Cività Cattolica" anawaalika wasomaji wake katika kipindi hiki
cha Majilio kutafakari kwa kina na mapana baadhi ya mahubiri yaliyowahi kutolewa na
Baba Mtakatifu Francisko katika utume na maisha yake kwa kuangalia mwanga wa Noeli,
ili waamini waweze kuwa kweli ni watoto wa mwanga unaowaamsha kufikiri na kutenda
kama Watoto wa Mungu.
Mwana wa Mungu ambaye alifanyika Mwanga ili kufukuza
giza katika maisha ya mwanadamu si mwanga unaotisha, lakini ni angavu na uko karibu
sana na maisha ya mwanadamu. Huu ni mwanga unaochochea toba na wongofu wa ndani katika
maisha ya mwamini, ili kamwe asimezwe na malimwengu.
Baba Mtakatifu Francisko
anawaalika waamini kuwa kweli ni Watoto wa Mwanga, ili waweze kutembea katika mwanga
wa utakatifu wa maisha, mwaliko wa kwanza kwa kila Mkristo, kwani wanapomwona Mtoto
Yesu akiwa amelazwa kwenye Pango la kulishia wanyama, hapo wanaweza kuonja ukuu na
utukufu wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.
Mwanga unaoletwa na Neno wa Mungu
aliyefanyika mwili unawamsha waamini kutoka katika usingizi, ili kuwasaidia kutembelea
katika dunia hii kwa moyo wa unyenyekevu, huku wakiendelea kukua na kuongezeka katika
kimo na busara kama ilivyokuwa kwa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Majilio na hatimaye
Siku kuu ya Noeli ni kipindi cha matumaini na mwanzo wa maisha mapya yanayojikita
katika huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Huu ni mwendelezo
wa mchakato wa majiundo endelevu katika azma ya Uinjilishaji mpya unaojikita katika
ushuhuda wa imani inayomwilishwa katika matendo ya huruma na mapendo.
Katika
kipindi cha Majilio, Mama Kanisa anapenda kumwonesha kwa namna ya pekee Mtakatifu
Yosefu, Baba Mlishi wa Yesu, aliyejitaabisha kuhakikisha kwamba, Familia Takatifu
inapata mahitaji yake msingi, huku akijiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu ili aweze
kumwongoza kadiri ya mpango na haki yake ya Kimungu, tofauti kabisa na haki ambayo
wakati mwingine binadamu anapenda kumsingizia Mungu, changamoto kwa Wakristo kujisadaka
kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya jirani zao.
Yesu alizaliwa mjini Bethelehemu,
Nyumba ya Mkate, pembezoni mwa Utawala wa Kirumi, ndivyo Mwenyezi Mungu katika Fumbo
la Umwilisho, amependa kujinyenyekesha na kuzaliwa kama binadamu, lakini zaidi katika
Pango la kulishia wanyama. Noeli ni Siku kuu inayoonesha ukuu na utukufu wa Mungu
katika mambo ya kawaida. Hapa mwamini anajifunza kwamba, Mwenyezi Mungu anatekeleza
mpango wa ukombozi wa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti kwa njia ya
Fumbo la Umwilisho.