Ekaristi Takatifu ni chemchemi ya matumaini na mkate wa unaozima kiu ya maisha ya
kiroho!
Ekaristi Takatifu ni Fumbo linalozima kiu ya maisha ya kiroho kwa mwamini na hivyo
kumkirimia nguvu ya kuweza kusonga mbele kwa imani, matumaini na mapendo. Ekaristi
Takatifu inaonesha uwamo wa Kristo katika maumbo ya mkate na divai, mwamba thabiti
wa imani, kwa mwamini anayethubutu kumkimbilia Yesu, ili kumwabudu, kumwomba na kumsujudu
katika maisha yake.
Kipindi cha
Majilio ni nafasi murua ya kutambua uwepo endelevu wa Kristo katika hija ya maisha
ya waamini na kwamba, kipindi hiki mara nyingi kinahusishwa na maandalizi ya Siku
kuu ya Noeli, yaani kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa Dunia. Yote haya ni kweli,
lakini, Kipindi cha Majilio ni mwaliko kwa waamini kuvunja tabia ya mazoea katika
masuala ya kidini na kuanza kujikita zaidi katika imani inayowaonesha uwepo wa Mungu
kati yao, changamoto ya kumwilisha imani katika uhalisia wa maisha, kwani Mungu yupo
pamoja na watu wake.
Hivi ndivyo Askofu msaidizi Lorenzo Leuzzi wa Jimbo kuu
la Roma anavyowaandikia wanafunzi Wakristo wanaosoma katika taasisi za elimu na vyuo
vikuu mjini Roma katika kipindi hiki cha Majilio. Imani inapata chimbuko lake katika
Fumbo la Utatu Mtakatifu, ndiyo maana Mama Kanisa anawakumbusha waamini kwamba, Neno
wa Mungu, aliyefanyika mwili na kukaa kati ya watu wake, ndiye Yesu Kristo Mkombozi
wa dunia, aliyezaliwa duniani yapata miaka elfu mbili iliyopita.
Yesu Kristo
yupo ndani ya Kanisa lake kwa njia ya Neno la Mungu na Sakramenti za Kanisa. Yesu
atakuja tena kuwahukumu wazima na wafu na wala ufalme wake hautakuwa na mwisho. Waamini
wanatambua kwamba, Yesu alizaliwa mjini Bethlehemu, “Nyumba ya Mkate”, yeye ndiye
sababu ya matumaini yasiyodanganya kamwe, kwani atawawezesha waamini kufikia utimilifu
wa maisha.
Askofu msaidizi Leuzzi anawakumbusha wanafunzi kwamba, kwa bahati
mbaya wakristo nao wamekumbwa na “ugonjwa wa kukosa uvumilivu” ni watu wenye haraka
zao, hawana tena subira, wanapelekwa mchakamchaka na maendeleo ya sayansi na utandawazi
kana kwamba, ni daladala iliyokatika usukani. Ndiyo maana, Kipindi cha Majilio, kinawaalika
waamini kuvuta subir a pamoja na kuwa na matumaini, huku wakimwomba, Yesu kuwapatia
chakula cha uzima wa milele, Mkate ulioshuka kutoka mbinguni.
Huu ni Mkate
wa matumaini, unaowachangamotisha waamini kuwa imara na thabiti katika imani, matumaini
na mapendo! Kusimika maisha yao kwa Kristo na Kanisa lake bila ya kuyumba wala kuyumbishwa,
kwani inapendeza na inalipa kumtumainia Yesu Kristo! Waamini wanaalikwa kumkimbilia
Yesu, ili aweze kuzima kiu ya maisha yao ya kiroho na kuwaimarisha katika imani, tayari
kuishuhudia katika uhalisia wa maisha, kwa kuwakirimia furaha na maisha ya uzima wa
milele. Yesu ni dira na mwongozo thabiti wa maisha.
Kipindi cha Majilio, iwe
ni fursa makini ya kujiandaa kwa ajili ya kumpokea Neno wa Mungu aliyefanyika Mwili,
Yesu Kristo, Mkate ulioshuka kutoka mbinguni, kwani maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli
si kukumbuka mambo ya kale, lakini ni Siku kuu inayoonesha uwepo endelevu wa Yesu
Kristo Mwana wa Mungu kati ya watu wake; Yesu ambaye atakuja tena kuwahukumu wazima
na wafu na wala ufalme wake hautakuwa na mwisho. Huu ni mwaliko kwa Wakristo kujitahidi
kupokea Mkate wa uzima, unaozima kiu ya maisha ya uzima wa milele, tayari kujisadaka
kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.