2014-12-05 15:00:43

Biashara haramu ya binadamu inadharirisha utu na heshima ya binadamu!


Baba Mtakatifu Francisko amewapongeza wadau mbali mbali wanaoshiriki katika mkutano wa kimataifa wa kupambana na biashara haramu ya binadamu, unaofanyika mjini London, Uingereza kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 6 Desemba 2014. Hizi ni juhudi zinazopania kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kisheria ili kupambana na biashara haramu ya binadamu sanjari na kuwasaidia waathirika wa biashara hii.

Ujumbe wa Baba Mtakatifu uliotumwa kwa Kardinali Vincent Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza na Wales, umesomwa kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko na Askofu Marcelo Sanchez Sorondo, Mkuu wa Taasisi za Kipapa za Sayansi Jamii, anayeshiriki katika mkutano huu wa kimataifa unaowajumuisha Maaskofu, Wakuu wa Jeshi la Polisi nchini Uingereza pamoja na Kikundi cha Santa Marta, kilichoanza utume wake mjini Vatican, Mwezi Aprili 2014.

Baba Mtakatifu anasema, biashara haramu ya binadamu ina dharirisha utu na heshima ya binadamu na kwamba, anawashukuru wadau wote wanaojipanga barabara kuhakikisha kwamba, wanalivalia njuga tatizo hili la biashara haramu ya binadamu na kwamba, Kanisa litaendelea kuwa mstari wa mbele katika mapambano haya.







All the contents on this site are copyrighted ©.