Shirikisho la vyama vya kujitolea vya Kanisa Katoliki nchini Italia vina mchango mkubwa
katika kuwasaidia watu waliokumbwa na majanga mbali mbali duniani, Kanisa kwa upande
wake litaendelea kushikamana na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa
jamii. Shirikisho la vyama hivi ni mfano bora wa Wasamaria wema wanaotekeleza dhamana
na majukumu yao kwa kujikita katika tunu msingi za maisha ya Kiinjili, kwa kupambana
kikamilifu na baa la njaa na kashfa ya vita duniani.
Haya yamesemwa na Baba
Mtakatifu Francisko wakati alipokutana na kuzungumza na Shirikisho la Vyama vya Kujitoleavya
Kanisa Katoliki nchini Italia, FOSCIV, Alhamisi, tarehe 4 Desemba 2014 katika maadhimisho
ya Siku ya Kujitolea Duniani. Huduma yao ni kielelezo makini cha huruma na upendo
unaobubujika kutoka kwa Yesu anayeendelea kufanya hija na binadamu katika shida na
mahangaiko yake. Kuna haya ya watu kutolea ushuhuda wa sadaka kwa ajili ya maskini,
ili waweze kuwa na matumaini yanayofumbatwa katika mshikamano wa upendo. Watu wanaojitolea
ni vyombo vya huduma ya Jumuiya inayotolewa kwa ajili ya maskini.
Baba Mtakatifu
anasema, haitoshi kuwahudumia maskini tu, bali kujifunga kibwebwe ili kukata mzizi
wa fitina unaosababisha baa la umaskini; haya ni mambo yanayojikita katika ukosefu
wa usawa, fursa za ajira, makazi; ukosefu wa haki msingi za kijamii na katika maeneo
ya kazi. Mshikamano wa upendo na udugu ni njia makini ya kuandika historia mpya na
maskini, kwa kulinda na kutunza mazingira, kwani kazi ya uumbaji ni zawadi kubwa kutoka
kwa Mwenyezi Mungu inayopaswa kulindwa, kutunzwa na kuendelezwa na kwamba, hii ni
hazina inayopaswa kurithishwa kwa kizazi kijacho!
Baba Mtakatifu anasema, bado
kuna kashfa ya vita, inayowachangamotisha watu kushikiriana ili kujenga misingi ya
haki na amani; kwa kujenga na kuimarisha madaraja ya watu kukutana kidini na kitamaduni,
huku wakisindikizwa na imani wanapotekeleza wajibu wao katika mazingira magumu, kwani
kazi yao ni kielelezo makini cha amani na matumaini kwa wakimbizi na wahamiaji, wanaokimbia
dhuluma na nyanyaso za kidini; watu wanaotafuta maisha bora! Wafuasi wa Kristo wanapaswa
kuwasaidia watu hawa kwa kuwaonjesha ukarimu wa Kiinjili badala ya kuwageuzia kisogo.
Baba
Mtakatifu anawataka wanachama hawa kushirikiana na wadau mbali mbali ili kujenga na
kudumisha amani na utulivu kati ya watu wenye tamaduni tofauti, sanjari na kuokoa
maisha ya wahamiaji ili wasitumbukie na kufa maji baharini au katika mikono ya wafanyabiashara
haramu ya binadamu, watu ambao dhamiri zao zimekufa.
Miaka arobaini ya shughuli
za kujitolea si haba anasema Baba Mtakatifu, kwani wamejitahidi kuwa kweli ni mashahidi
wa upendo, vyombo vya ujenzi wa haki, amani na mshikamano, mwaliko wa kuendelea kutekeleza
utume huu kwa moyo wa furaha unaorutubishwa kwa sala ambayo inawategemeza wakati wanapokumbana
na magumu; wanapokata tamaa, wanaposhindwa kueleweka au wanapokumbwa na upweke hasi!
Na
Padre Ricard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.