2014-12-03 11:31:52

Tangazeni kwamba, Al Shabaab ni janga la kitaifa Kenya!


Askofu mkuu Zacchaeus Okoth, Mwenyekiti wa Tume ya haki na amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya ameitaka Serikali ya Kenya kutangaza kwamba, mashambulizi ya Al Shabaab ni janga la kitaifa pamoja na kufanya udhibiti mkubwa wa uuzaji wa silaha kwa raia, kama njia ya kupambana na mashambulizi ya kigaidi ambayo yameendelea kusababisha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia kwa misingi ya kidini.

Wananchi wanaendelea kuomboleza kwa kuondokewa na ndugu, jamaa na rafiki zao, kumbe umefika wakati kwa Serikali kutenda kwa ujasiri ili kuokoa maisha ya watu wasiokuwa na hatia yanayoendelea kupukutika kama majani makavu wakati wa kiangazi. Serikali itenge kikosi maalum kitakachokula sahani moja na kikundi cha kigaidi cha Al Shabaab, kinachofanya mauaji kwa misingi ya kidini. Serikali inawajibu wa kulinda raia na mali zao na kwamba, kwa sasa maeneo yaliyoko Kaskazini Mashariki mwa Kenya si salama kwa maisha ya raia na mali zao.

Rushwa ni chanzo kikuu cha Serikali kushindwa kutekeleza wajibu wake katika masuala ya ulinzi na usalama, changamoto kwa Serikali kuhakikisha kwamba, inafanya upembuzi yakinifu kuhusu watu wanaoteuliwa kufanya kazi katika vyombo vya ulinzi na usalama.







All the contents on this site are copyrighted ©.