Ilikuwa ni hija ya amani na majadiliano ya kiekumene!
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake, Jumatano tarehe 3 Desemba, 2014,
Kumbu kumbu ya Mtakatifu Francisko Xsaveri amefanya rejea katika hija yake ya kiekumene
nchini Uturuki, kuanzia tarehe 28 hadi tarehe 30 Desemba, Siku kuu ya Mtakatifu Andrea,
Mtume.
Baba Mtakatifu amemshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema na baraka alizomkirimia
wakati wa hija yake ya kiekumene nchini Uturuki. Anatumaini kwamba, majadiliano kiekumene
kati ya Wakristo na yale ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam yataendelea kuboresha
mahusiano na udugu kati ya waamini wa dini hizi. Uturuki ni nchi ambao ina utajiri
mkubwa wa kihistoria katika maisha na utume wa Kanisa. Maisha ya kiroho yana nafasi
ya pekee sana nchini Uturuki, ambayo kimsingi ina waamini wengi wa dini ya Kiislam.
Baba
Mtakatifu anasema, alipotembelea mjini Ankara, Uturuki, lengo lilikuwa ni kukazia
umuhimu wa kukuza na kudumisha uhuru wa kidini kwa wote pamoja na kuendeleza mchakato
wa majadiliano ya kiekumene ili kujenga na kudumisha mshikamano, haki na amani. Akiwa
Istanbul, wakati wa maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu na waamini wa Kanisa Katoliki
pamoja na viongozi kadhaa wa Jumuiya za Kikristo, kwa pamoja walimwomba Roho Mtakatifu,
kuendelea kuliongoza na kulisaidia Kanisa kukua na kuimarika katika umoja na uaminifu.
Baba
Mtakatifu Francisko anasema, kilele cha hija yake ya kiekumene nchini Uturuki, kilikuwa
ni hapo Jumapili tarehe 30 Desemba 2014, Siku kuu ya Mtakatifu Andrea, Mtume, alipounganika
na Patriaki Bartolomeo wa kwanza kusali na hatimaye, kutia sahihi tamko la pamoja
linalopania kuimarisha umoja wa Makanisa. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuendelea
kusali kwa ajili ya kuombea nia hii njema kwa Kanisa kutaka kutangaza Habari Njema
ya Wokovu; kuheshimiana na kuendeleza majadiliano ya kidugu, ili kumwilisha ujumbe
wa Kristo unaojikita katika ukweli, amani na upendo.
Baba Mtakatifu amewaambia
mahujaji kwamba, Kipindi cha Majilio, kiwasaidie kujiandaa kwa ajili ya ujio wa Yesu
Kristo Mfalme wa amani na kwamba, waendelee kusali ili hija yake ya kichungaji nchini
Uturuki ilete umoja na mshikamano kati ya Wakristo sanjari na amani huko Mashariki
ya Kati.
Majilio iwe ni fursa ya kushikamana na Yesu, kwa kuonesha mshikamano
wa upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Waamini wasali ili
kweli watu waweze kuishi kwa amani na utulivu, huku imani na mapendo vikimwilishwa
sanjari na kuwatangazia Watu wa Mataifa kwamba, Yesu Kristo ni njia, ukweli na uzima.
Baba
Mtakatifu anawakumbusha waamini kwamba, Roho Mtakatifu ndiye mhimili mkuu wa umoja
wa Kanisa; wamwombe ili asaidie kuonesha njia itakayowapeleka Wakristo katika umoja
kamili, unaomwilishwa katika maisha ya kila siku. Waamini waendelee kuungana naye,
ili kuwaombea Wakristo Mashariki ya Kati, waweze kuwa na imani thabiti, upendo na
matumaini na kwamba, uwepo wao kiwe ni kielelezo cha umoja na mshikamano wa kidugu.
Baba
Mtakatifu alipata nafasi ya kuwasalimia wagonjwa waliokuwa wanafuatilia Katekesi yake
kutoka kwenye Ukumbi wa Paulo VI ulioko mjini Vatican, kutokana na wasi wasi wa mvua
kubwa kunyeesha. Amewasihi kusali kwa ajili yake.