2014-12-02 12:11:13

Mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu Barani Ulaya!


Amini, usiamini lakini takwimu zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu laki nane ambao wametumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu katika nchi za Jumuiya ya Ulaya, jambo ambalo linadhalilisha utu na heshima ya watu hawa, ambao wengi wao ni wale wanaotoka katika mazingira hatarishi zaidi.

Haya yamebainishwa hivi karibuni na Tume ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki kwenye Jumuiya ya Ulaya, COMECE wakati wa majadiliano yaliyokuwa yanaongozwa na kauli mbiu "Kanisa na Jamii yaliyofanyika mjini Brussels, Ubelgiji.

COMECE katika taarifa yake baada ya majadiliano haya inaonesha kwamba, asilimia 60 ya waathirika wa biashara haramu ya binadamu wanatoka katika nchi zinazounda Jumuiya ya Umoja wa Ulaya, changamoto ya kukuza na kuendeleza ushirikiano kati ya Serikali, vyama vya kiraia na Kanisa ambalo limekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu ambayo ni kielelezo cha mwendelezo wa utumwa mamboleo na uhalifu wa kimataifa. Biashara hii haramu inaendelea kushamiri sehemu mbali mbali za dunia kiasi cha kushika nafasi ya tatu kimataifa baada ya biashara haramu ya dawa za kulevya na silaha duniani.

Watu wanaotumbukizwa kwenye biashara haramu ya binadamu; wanawake, wasichana na watoto wanafanyishwa biashara ya ukahaba; baadhi yao wanafanyishwa kazi za suluba kwa kulipwa "kiduchu"; baadhi ya wanawake wanabebeshwa mimba za chupa pamoja kuasi watoto kinyume cha sheria. Takwimu zinaonesha kwamba, asimilia 16% ya watoto wenye umri mdogo wanauzwa kwa Euro arobaini elfu kwa kila mtoto, matendo ya aibu kabisa.

Wajumbe wa semina hii wameiomba Jumuiya ya Ulaya kuhakikisha kwamba, inakusanya takwimu kwa uhakika ili kupambana kikamilifu dhidi ya biashara haramu ya binadamu pamoja na kuendelea kuwasaidia waathirika wa mchezo huu mchafu. Hili kundi ambalo linapaswa kulindwa na kuthaminiwa, lakini wakati mwingine wahanga wa biashara haramu ya binadamu wamekuwa wakiadhibiwa wanapopatikana na makosa kama haya. Jumuiya ya Umoja wa Ulaya ishirikiane kwa karibu zaidi na vyama vya kiraia, asasi pamoja na Kanisa katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.