2014-12-02 08:56:58

Asante Papa Francisko, makali yako tumeyaona!


Baraza la Maaskofu Katoliki Uturuki linamshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kufanya hija ya kiekumene nchini mwao, kwa kupata fursa ya kukutana, kuzungumza na kusali pamoja na Patriaki Bartolomeo wa kwanza pamoja na kuitia shime Familia ya Mungu nchini Uturuki, hata katika uchache wao. Hija hii imekuwa ni kikolezo cha ujasiri unaojikita katika matumaini, ili kuweza kukabiliana na changamoto za ushuhuda wa maisha ya Kikristo nchini Uturuki.

Baraza la Maaskofu Katoliki Uturuki, linamshukuru Baba Mtakatifu kwa kuwaonesha njia ya majadiliano ya kiekumene na kidini na waamini mbali mbali wanaoishi nchini Uturuki. Wakatoliki wanapenda kuendeleza mwaliko uliotolewa na Baba Mtakatifu unaowataka kufahamiana, kuheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana katika hija ya maisha yao hapa duniani; kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mambo yale yanayowaunganisha zaidi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Uturuki linamshukuru Baba Mtakatifu kwa kuonesha ukweli kwamba, amani ya kweli inajikita katika kuheshimu haki msingi, utu na heshima ya binadamu. Familia ya Mungu nchini Uturuki, inapenda kuwa ni mdau mkuu katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene, kidini na kitamaduni, kwa kutoa msukumo wa pekee katika mshikamano wa upendo kati ya wananchi wa Uturuki, ili kujenga na kudumisha amani na utulivu kati ya watu. Familia ya Mungu nchini humo inapenda kumhakikishia Baba Mtakatifu Francisko kwamba, itaendelea kumsindikiza katika maisha na utume wake kwa njia ya sala na bado wanamwomba aendelee kuiombea Uturuki na watu wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.