2014-12-01 11:47:23

Siku ya Ukimwi Duniani 2014


Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis katika maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani inayoadhimishwa na Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe Mosi, Desemba linasema kwamba, kila mtu anapaswa kupata maisha bora na kuhudumiwa kwa heshima ya tahadhima, changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema!

Lengo hili linaweza kufikiwa ikiwa kama jamii itafanikiwa kuvunjilia mbali kuta za utengano kwa kuwakumbatia wote wenye shida na mahangaiko yao ndani; kwa kuheshimu na kuthamini utu wao kama binadamu pamoja na kuwahudumia kwa moyo wa upendo na huruma.

Takwimu zinaonesha kwamba, kuna watu zaidi ya millioni 39 waliofariki kutokana na ugonjwa wa Ukimwi pamoja na magonjwa mengine nyemelezi katika kipindi cha miaka thelathini iliyopita. Caritas Internationalis, wakati wote huu, imetembea na waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi kwa kuwajengea uwezo, ili kukabiliana kikamilifu na changamoto za maisha, changamoto ya kuendelea kuboresha huduma kwa waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi pamoja na kupunguza maambukizi mapya; kwa kuonesha mshikamano pamoja na kutafuta mafao ya wengi pamoja na kutoa dawa za kurefusha maisha kwa wagonjwa wapatao millioni 25; kwa kuendelea kuzuia maambukizi mapya; kwa kuwaonesha upendo wagonjwa na waathirika wa Ukimwi pamoja na kuwahudumia wahamiaji na wakimbizi ambao wakati mwingine inakuwa ni vigumu kwao kupata huduma za afya.

Kipaumbele cha kwanza kiwe ni kwa ajili ya watoto, kwa kuwapatia huduma zitakazozuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto wakati wa kujifungua pamoja na kupambana na umaskini, ili watu wengi waweze kupata dawa za kurefusha maisha, huku utu wao ukiheshimiwa na kuthaminiwa,kwa kuongozwa na kanuni ya upendo kwa Mungu na jirani.







All the contents on this site are copyrighted ©.