Papa arejea mjini Vatican baada ya hija yake ya kiekumene nchini Uturuki
Mara baada ya kuhitimisha hija yake ya kiekumene nchini Uturuki, iliyomwezesha kukutana
na kusali na waamini wa dini mbali mbali nchini Uturuki, ili kujenga udugu na umoja,
haki na amani miongoni mwa jamii, Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili alasiri tarehe
30 Novemba 2014 alifunga vilago na kurejea tena mjini Vatican. Lakini kabla ya kuondoka
kurejea Vatican, Baba Mtakatifu alimtembelea na kumsalimia Patriaki Mesrob Mutafian
wa Kanisa la Kiarmeni la Costantinopol, ambaye ni mgonjwa sana na amelazwa kwenye
Hospitali ya San Salvatore mjini Istanbul, Uturuki.
Akiwa njiani, amewatumia
ujumbe wa matashi mema Marais wa Ugiriki, Albania na Italia. Akiwa kwenye hanga za
Ugiriki, Baba Mtakatifu amemtakia Rais Karolos Papoulias baraka za mshikamano na amani
kwa wananchi wa Ugiriki. Baba Mtakatifu katika ujumbe wake kwa Rais Bujar Nishani
wa Albania, amewatakia amani, neema na baraka anaporejea kutoka katika hija yake ya
kiekumene nchini Uturuki.
Baba Mtakatifu amemwambia Rais Giorgio Napolitano
wa Italia kwamba, akiwa nchini Uturuki, amebahatika kukutana na kuzungumza na makundi
mbali mbali ya wananchi wa Uturuki na amewaonesha moyo wake wa shukrani, hasa kutokana
na utajiri mkubwa unaofumbatwa katika historia na maisha ya wananchi wa Uturuki. Amewasihi
kuendeleza mchakato wa kujenga na kudumisha misingi ya haki na amani, kwa njia ya
majadiliano ya kidini na kiekumene. Anawatakia wananchi wote wa Italia umoja na mshikamano
wa kweli.
Akiwa angani, Baba Mtakatifu Francisko alipata nafasi ya kuzungumza
na waandishi wa habari kuhusu hija yake ya kiekumene pamoja na kujibwa maswali kadhaa,
mazungumzo ambayo yamedumu kwa takribani masaa matatu na robo!
Baba Mtakatifu
Francisko alipowasili jioni kwenye Uwanja wa ndege wa Ciampino amepokelewa na viongozi
mbali mbali wa Kanisa na Serikali ya Italia na baadaye akaelekea moja kwa moja kwenye
Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu, kummshukuru Bikira Maria aliyemsimamia na kumwongoza
katika hija yake ya kiekumene nchini Uturuki.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.