2014-11-30 11:37:07

Watawa jikiteni katika Injili, Unabii na Matumaini!


Kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko, Kardinali Joao Braz de Avis, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume, Jumapili tarehe 30 Novemba 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuzindua Mwaka wa Watawa Duniani utakaofikia kilele chake hapo tarehe 2 Februari 2016, kwa kuwataka watawa kujikita zaidi na zaidi katika Injili; Utume na Unabii, huku wakijiaminisha chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa.

Kardinali De Avis anasema, Baba Mtakatifu Francisko alitamani kuwepo kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro hapa mjini Vatican kwa ajili ya kuzindua Mwaka wa Watawa, lakini kutokana na uzito wa hija ya kiekumene, hakufanikiwa, lengo ni kuendeleza majadiliano ya kiekumene na kidini kati ya waamini wa dini mbali mbali, ili kujenga na kudumisha mshikamano wa dhati.

Nia ya Baba Mtakatifu katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa ni kuhakikisha kwamba, watawa wanaendelea kujitosa bila ya kujibakiza kwa kuonesha upendo wao kwa Mwenyezi Mungu, huku wakikumbatia Mashauri ya Kiinjili, ambayo ni: Ufukara, usafi kamili na utii. Kanisa linauzindua Mwaka wa Watawa kwa kuonesha matumaini yake kwa Mwenyezi Mungu ambaye daima amekuwa mwaminifu na mwingi wa huruma na mapendo; anayebatilisha ukosefu wa uaminifu kwa njia ya huruma yake na kwamba, mtu anayemtumaini kamwe hataweza kudanganyika.

Kardinali De Avis anasema, hata watawa wanapaswa kujisikia kutoka katika undani wa maisha yao kwamba, wanahitaji kuonja huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kama ilivyokuwa kwa Waisraeli wanaosimuliwa katika Liturujia ya Neno la Mungu, kwa kumwonesha Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, ili kuwa karibu zaidi na binadamu na watawa wanayo kila sababu ya kusema, " Ee Bwana, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu, sisi sote tu kazi ya mikono yako." Na Mwinjili Marko anawataka waamini kukesha na kusali; mambo msingi katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani.

Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake kwa Watawa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa inayojulikana kama "Mashahidi wa Furaha", anawataka watawa kuwa kweli ni chemchemi ya furaha, wakionesha kwamba, Mwenyezi Mungu anaweza kuwakirimia furaha ya kweli bila ya kuwa na kishawishi cha kutafuta furaha hii mahali pengine popote.

Baba Mtakatifu anasubiri kwa hamu kuona watawa wakiwaamsha walimwengu kwa njia ya Unabii, kwa kujikita katika Injili, changamoto kwa Familia nzima ya Mungu, lakini watawa wanawajibika zaidi kwani wao wamechagua kuacha yote kwa ajili ya Mungu na jirani. Watawa wawe ni mashahidi wanaoshuhudia maisha ya Yesu hapa duniani na kwamba, hiki ni kipaumbele cha pekee kwa watawa.

Watawa wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuwa ni wataalam wa umoja, unaojidhihirisha katika maisha ya kiroho kwa kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoibuliwa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, ili kweli Kanisa liweze kuwa ni nyumba na shule ya umoja.

Ni mwaliko kwa watawa kutoka katika ubinafsi wao, ili kwenda pembezoni mwa maisha ya watu ndani ya jamii, kwani watu wengi bado wanangojea kusikia Habari Njema ya Wokovu, sanjari na kusoma alama za nyakati ili kujibu kilio cha damu kutoka kwa watu wa nyakati hizi, daima kwa kumsikiliza Roho Mtakatifu, ili kweli Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani kiwe ni kipindi cha wongofu, neema na mabadiliko ya kweli, daima wakiwa na ujasiri.

Haya ndiyo mambo msingi yanayopaswa kufanyiwa kazi katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani anasema Kardinali Joao Braz de Avis, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume katika mahubiri kwenye Ibada ya kufungua Mwaka wa Watawa Duniani 2014 hadi mwaka 2016.







All the contents on this site are copyrighted ©.