2014-11-30 10:11:24

Viongozi wenye uchu wa madaraka watapambana na nguvu ya umma!


Rais Francois Hollande wa Ufaransa, amewaonya viongozi Barani Afrika wanaotaka kung'ang'ania madarakani kwa kupindisha Katiba kwamba, watapambana na nguvu ya umma kama ilivyojitokeza huko Burkina Faso, kwa kumng'oa kutoka madarakani Rais Blaise Compaore aliyetawala kwa kipindi cha miaka 30 lakini bado alitaka kung'ang'ania madarakani. Tukio hili liwe ni fundisho kubwa kwa viongozi wenye uchu wa madaraka. Rais Hollande ameyasema haya mwishoni mwa juma, wakati alipokutana na viongozi wakuu wa nchi za Afrika Magharibi.

Katiba za nchi nyingi Barani Afrika zimeweka vipindi viwili kwa Rais kuweza kukaa madarakani na muda huu unapomalizika, awe radhi kung'atuka kutoka madarakani, lakini baadhi ya Marais wamekuwa na kishawishi cha kutaka kupindisha Katiba za nchi ili waendelee kubaki madarakani. Cameroon na Togo ni nchi ambazo zineonesha dalili za kutumbukia kwenye kishawishi hiki.

Ufaransa inasema, itashikamana na nguvu ya umma kuwaondoa madarakani viongozi wanaong'ang'ania kubaki madarakani kwa kupindisha Katiba na Sheria za nchi, kwani kwa kufanya hivi, viongozi kama hawa wanahatarisha uhuru wa wananchi.







All the contents on this site are copyrighted ©.