2014-11-29 12:11:32

Misimamo mikali ya kiimani na uhalifu kwa jina la kidini ni mambo ambayo hayawezi kukubalika!


Majadiliano ya kidini kati ya Kituo cha Majadiliano na utamaduni wa dini ya Kiislam na Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini, yaliyokuwa yanafanyika mjini Teheran kwa kuongoza na kauli mbiu "Wakristo na Waislam katika majadiliano kwa ajili ya mafao ya kijamii" umehitimishwa kwa washiriki kutoa tamko la pamoja linalopongeza juhudi ambazo zimefikiwa hadi sasa katika kujenga na kuimarisha mahusiano kati ya pande hizi mbili.

Dr. Abuzar Ibrahimi Turkaman aliongoza ujumbe kutoka upande wa waamini wa dini ya Kiislam na Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini, aliongoza ujumbe kutoka Vatican. Mkutano huu wa siku mbili umepongeza jitihada za makusudi baina ya waamini kutaka kufahamiana zaidi na hatimaye kujenga jamii yenye amani, upendo na mshikamano.

Wajumbe hawa wamelaani kwa kauli moja misimamo mikali ya kiimani pamoja na vitendo vyote vya uhalifu kwa misingi ya kidini, kuwa ni mambo ambayo hayawezi kukubalika. Wajumbe hawa watakutana tena mjini Roma kunako mwaka 2016, lakini mwaka 2015 utakuwa na vikao vya maandalizi ya pamoja.







All the contents on this site are copyrighted ©.