2014-11-28 08:26:58

Siku ya mshikamano wa kimataifa na Wananchi wa Palestina


Bado kuna kinzani na migogoro mikubwa kati ya Palestina na Israeli, kiasi cha kugumisha mchakato wa kutafuta amani hasa kwenye Ukanda wa Ghaza, changamoto kwa pande hizi mbili kusitisha vita na kuendeleza majadiliano ya amani na upatanisho.

Umoja wa Mataifa unalaani mashambulizi ya makombora yanayofanywa na Hamas dhidi ya raia wa Israeli, mambo yanayosababisha mateso na mahangaiko makuba kwa watu wasiokuwa na hatia. Mashambulizi yaliyofanywa na Israeli huko Palestina yamesababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao, mwaliko kwa Israeli kuwajibika barabara katika maamuzi yake sanjari na kulinda haki msingi za binadamu kimataifa.

Hii ni sehemu ya ujumbe kutoka kwa Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Wapalestina, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 29 Novemba. Amani na utulivu anasema Katibu mkuu, vinategemea kwa namna ya pekee kabisa utashi kutoka kwa pande zote mbili; kwa kuheshimu sheria za kimataifa sanjari na Israeli kuacha ujenzi wa makazi katika maeneo ya Palestina.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anawakumbuka kwa namna ya pekee, wakimbizi kutoka Palestina wanaoishi kwenye Ukanda wa Ghaza na kwingineko. Anawapongeza wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa wanaowahudumia wakimbizi huko Mashariki ya Kati pamoja na kusaidia mchakato wa ujenzi wa Gaza, ingawa hali bado si shwari sana huko Yerusalem. Hapa kuna haja kwa pande hizi mbili kuheshimiana na kuacha kuendeleza ujenzi usio halali kwenye makazi ya Wapalestina.

Mgogoro kati ya Palestina na Israeli utamalizika, ikiwa kama kutakuwepo na utashi wa kisiasa unaozingatia misingi ya usawa, majadiliano pamoja na kusimamia maafikiano yaliyokwisha kutolewa na Umoja wa Mataifa. Waisraeli na Wapalestina wanategemeana na hivyo wanapaswa kuishi kwa kuvumiliana kwani wanahitajiana. Siku ya mshikamano na Wananchi wa Palestina iwatie shime viongozi wa Israeli na Palestina kuachana na falsafa ya kulipizana na kisasi na kujikita katika mchakato wa ujenzi misingi ya haki na amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.