2014-11-27 08:07:19

Maisha ya Kitawa, Injili na Matumaini!


Askofu mkuu Josè Rodriguez Carballo, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya kitawa na kazi za kitume anasema kwamba, maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani yataanza kutimua vumbi hapo tarehe 30 Novemba 2014, Jumapili ya kwanza ya Majilio, kipindi cha matumaini na kuhitimishwa rasmi tarehe 2 Februari 2016, Siku ya Watawa Duniani. RealAudioMP3

Hiki ni kipindi chenye utajiri mkubwa katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kuangalia umuhimu na mchango wa Watawa katika mchakato wa Uinjilishaji mpya; fursa zilizopo na changamoto mbali mbali zinazowakabili watawa sehemu mbali mbali za dunia.

Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani ni mwendelezo wa mchakato wa hija ya maisha ya Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo, changamoto iliyofanyiwa kazi kwa namna ya pekee na Mtakatifu Yohane Paulo II, kwa kuangalia changamoto zilizopita, hali ya sasa ya maisha na utume wa Kanisa na kujiwekea mikakati ya shughuli za kichungaji kwa siku za usoni. Kanisa linapenda kuyaangalia maisha na utume wa watawa ndani ya Kanisa tangu baada ya maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Hiki ni kipindi cha kumkshukuru Mungu kwani kumekuwepo na maendeleo pamoja na mchango mkubwa uliotolewa na watawa ndani ya Kanisa, ili kwa mara nyingine tena watawa waweze kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa kusema, “tazama inavyopendeza kuwa mtawa ili kumfuasa Yesu na kuwatumikia jirani bila ya kujibakiza”!

Kwa njia hii, Mama Kanisa anapenda kuimarisha mikakati ya shughuli za kichungaji katika kukuza na kuimarisha miito ya kitawa ndani ya Kanisa. Hapa Kanisa linaialika Familia ya Mungu kutafakari juu ya “Maisha ya kitawa: injili; Unabii na Matumaini ndani ya Kanisa”.

Maadhimisho haya katika ngazi ya kimataifa anasema Askofu mkuu Carballo ni kuanzia tarehe 22 hadi tarehe 24 Januari 2015, maadhimisho haya yatakuwa na sura ya kiekumene. Katika maadhimisho ya Siku kuu ya Pasaka kuanzia tarehe 8 hadi tarehe 11 Aprili, 2015 kutafanyika kongamano la walezi. Tarehe 23 hadi tarehe 26 Septemba kutafanyika kongamano la watawa vijana, watakaowasha moto wa Injili mjini Roma kwa kuwashirikisha vijana wenzao uzuri wa kutangaza Injili katika maisha ya kitawa na kazi za kitume.

Mwishoni mwa Januari 2016 kutafanyika kongamano la watawa na mashirika ya kazi za kitume kwa kuwashirikisha Marais wa Mashirikisho ya Mabaraza ya Mashirika ya Kitawa na kazi za kitume kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Katika matukio yote haya kunatarajiwa uwepo wa Baba Mtakatifu aidha kwa kuadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu au kwa njia ya kukutana na kuzungumza na makundi haya.

Baraza la Kipapa la Mashirika ya kitawa na kazi za kitume linasema kwamba, maadhimisho ya Mwaka wa watawa Duniani ni tukio litakaloyashirikisha pia Mabaraza mengine ya kipapa, Shirikisho la wakuu wa Mashirika ya Kitawa pamoja na Vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa.

Askofu mkuu Carballo anasema, mkutano mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na kazi za kitume utafanyika kuanzia tarehe 25 hadi tarehe 29 Novemba 2014 kwa kuongozwa na kauli mbiu “Divai Mpya katika Viriba Vipya”, ni mwaliko wa kusikiliza hija ya maisha ya watawa mintarafu mwongozo wa Roho Mtakatifu, changamoto kwa watawa kuendelea kuwa waaminifu katika karama za mashirika yao sanjari na kusoma alama za nyakati.

Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani ni tukio la Kikanisa, kumbe, Makanisa mahalia kwa kushirikiana kwa karibu zaidi na watawa wanaweza kujipangia ratiba itakayowawezesha kuadhimisha Mwaka wa Watawa Duniani kwa ari na moyo mkuu.

Askofu mkuu Carballo anasema kwamba, kongamano la watawa mintarafu mwelekeo wa kiekumene ni mwaliko wa kujichotea utajiri mkubwa unaofumbatwa katika maisha ya kitawa na kazi za kitume kutoka kwenye Makanisa ya Mashariki. Hapa ni mahali pa kufanya upembuzi yakinifu ili kuibua utajiri huo ambao pia unahitajika kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa zima, ili kuendeleza majadiliano ya kiekumene yanayojikita katika maisha ya kiroho. Watawa wanaweza kutoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa dhamana hii, ili wote wawe wamoja chini ya mchungaji mmoja yaani Yesu Kristo!

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuhimiza umuhimu wa majiundo makini kwa Makleri na watawa ndani ya Kanisa. Mwaka wa Watawa Duniani itakuwa ni fursa ya kupembua kwa kina na mapana mikakati ya malezi kwa kuimarisha na kuboresha pale itakapoonekana inafaa zaidi. Ni mwaka unaomwangali mtawa kama binadamu kamili katika mahitaji yake msingi: kiroho na kimwili, mitarafu mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Watawa hawana budi kujenga na kuimarisha mahusiano yao na Yesu Kristo kwa njia ya Sakramenti, Tafakari ya Neno la Mungu linalomwilishwa katika imani tendaji. Kwa maneno mafupi, watawa wanaalikwa kuwa ni mashahidi wa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya maisha na utume wao. Maisha ya kijumuiya ni kati ya mambo ambayo yataendelea kuwekewa msisitizo wa pekee, ili kujenga na kudumisha upendo, umoja na udugu katika Kristo.

Maisha ya kitawa hayana budi kukumbatia na kumwilisha Mashauri ya Kiinjili: Yaani: utii, ufukara na useja, kama kielelezo makini cha unabii na mwaliko wa kuuamsha ulimwengu, kama alivyokazia Baba Mtakatifu Francisko alipokutana na kuzungumza na Wakuu wa Mashrika ya Kitawa, hii ikawa ni chemchemi ya maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani.

Ni changamoto na mwaliko kwa Mashirika ya kitawa na kazi za kimissionari sehemu mbali mbali za dunia kuhakikisha kwamba, yanamwilisha karama na utume wao mahali wanapoishi na kufanya kazi kwa kutambua kwamba, utamadunisho wa karama za Mashirika ya kitawa na kazi za kitume bado ni changamoto pevu kwa mashirika mengi!

Baraza la Kipapa la Mashirika ya kitawa na kazi za kitume linataka kuanzisha majiundo awali na endelevu kwa watawa kwa njia ya mitandao ya kijamii. Watawa wanaalikwa kuanzisha mnyororo wa sala kwa ajili ya kuliombea Kanisa, maisha ya kitawa na ulimwengu katika ujumla wake. Baraza pia linapitia nyaraka mbali mbali zinazogusia moja kwa moja maisha ya kitawa na kazi za kitume ndani ya Kanisa.

Kwa ufupi anasema Askofu mkuu Josè Rodrguez Carballo, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani ni moto wa kuotea mbali!

Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.