Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani yanakwenda sanjari na Jubilee ya miaka 50 tangu
Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipochapisha Waraka kuhusu Fumbo la Kanisa,
Lumen Gentium, inayojulikana kama Mwanga wa Mataifa, Kanisa kama Fumbo la Mwili wa
Kristo; linaloonekana na lile lisiloonekana; umuhimu wa Taifa la Mungu katika kushiriki
katika maisha na utume wa Kanissa pamoja na kukuza ari na moyo wa kimissionari.
Mama
Kanisa pia anaadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa
Vatican walipotoa Tamko kuhusiana na Maisha ya Kitawa: Perfectae Caritatis, yaani
Upendo Mkamilifu, Waraka uliowataka Watawa kupyaisha maisha yao, kwa kutoa nafasi
ya kwanza katika maisha ya kiroho, mashauri ya Kiinjili, maisha ya kijumuiya pamoja
na malezi makini kwa wale wote wanaotaka kujisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa
lake.
Haya ni matukio makuu yatakayoliwezesha Kanisa kufanya tafakari ya kina
katika maisha na utume wa Watawa sehemu mbali mbali za dunia. Mwaka wa Watawa Duniani
unazinduliwa rasmi, Jumamosi jioni tarehe 29 Novemba 2014 kwenye Kanisa kuu la Bikira
Maria Makuu, lililoko mjini Roma kwa Ibada na Mkesha wa Sala, kuanzia saa 1:00 Usiku.
Tarehe 30 Novemba, 2014, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, kutafanyika Ibada
ya Misa Takatifu kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, kuanzia
saa 4:00 asubuhi kwa saa za Ulaya.
Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa
na Kazi za Kitume linasema kwamba, matukio haya ni muhimu sana katika uzinduzi wa
Mwaka wa Watawa Duniani, kwa kujiweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria,
Mama wa Mungu na msimamizi wa maisha ya kitawa. Hiki ni kipindi cha matumaini, sala
na tafakari ya kina kuhusu matendo makuu ya Mungu katika maisha ya Watawa wanaoendelea
kujisadaka kwa ajili ya Mungu na jirani zao, kwa kutambua kwamba, imani ni zawadi
kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ambayo Watawa wanapenda kuwamegea na kuwashirikisha wengine.
Makanisa
mahalia sehemu mbali mbali za dunia, yataadhimisha Ibada ya Misa na kufanya mikesha
ya sala na tafakari kama sehemu ya mchakato wa uzinduzi wa Mwaka wa Watawa Duniani,
uliotangazwa na Baba Mtakatifu Francisko. Waamini wanaalikwa kusali na kumwomba Roho
Mtakatifu ili aweze kulikirimia Kanisa neema na baraka ili kujenga na kulipyaisha
Kanisa katika maisha na utume wake.