2014-11-25 08:11:24

Mchakato wa mabadiliko mjini Vatican umefikia hatua nzuri!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu, 24 Novemba 2014 amekutana na kuzungumza na Wakuu wa Mabaraza ya Kipapa mjini Vatican, ili kufafanua kwa kina na mapana hatua ambazo zimekwishafikiwa katika mchakato wa kufanya mabadiliko ya kina kwenye Makao makuu ya Vatican kama walivyopendekeza Makardinali katika mikutano yao elekezi kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, uliofanyika mwezi Machi, 2013.

Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican anasema, mkutano huu umedumu kwa takribani masaa matatu na hotuba ya ufunguzi imetolewa na Askofu Marcello Semeraro, Katibu wa Baraza la Makardinali, lililoundwa na Baba Mtakatifu Francisko, mwaka 2013 ili kumsaidia katika kuongoza Kanisa la Kristo pamoja na kupitia upya mkakati wa kiuchungaji uliobainishwa kwenye Waraka wa Kichungaji, "Pastor bonus" Mchungaji mwema.

Askofu Semeraro amefafanua mambo msingi yanayopaswa kufanyiwa kazi katika mchakato wa mabadiliko ya Makao makuu ya Vatican. Wakuu wa Mabaraza ya Kipapa na vitengo mbali mbali wamechangia mawazo na mang'amuzi yao na kwamba, Baraza la Makardinali linatarajiwa kufanya vikao vyake kuanzia tarehe 9 hadi tarehe 11 Desemba 2014 hapa mjini Vatican.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.