Kanisa bado lina mchango wa pekee katika ujenzi wa Jumuiya Ulaya
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Baba Mtakatifu
Francisko hapo tarehe 25 Novemba 2014 anatarajiwa kufanya hija yake ya kikazi mjini
Strasbourg, ili kuzungumza na wajumbe wa Bunge la Ulaya pamoja na Baraza la Ulaya,
baada ya kupita takribani miaka 26 tangu Mtakatifu Yohane Paulo II alipotembelea na
kuzungumza na wajumbe wa taasisi hizi, huku akisisitizia umuhimu wa kushikamana kulinda
na kutunza mazingira, kuwahudumia wahamiaji na wakimbizi pamoja na kuwa na mwono sahihi
wa binadamu.
Kardinali Parolin anasema, haya ni mambo ambayo bado ni changamoto
endelevu inayovaliwa njuga na Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba zake mbali mbali.
Anasema, umoja na mshikamano ni tunu msingi zinazounganisha Nchi za Umoja wa Ulaya
na kwamba, zinapaswa kuwa na mwelekeo sahihi juu ya binadamu na haki zake msingi pamoja
na kukabiliana na changamoto zinazotaka kudhalilisha utu na heshima ya binadamu.
Taasisi
za Ulaya hazina budi kutoa majibu sahihi kwa kero na changamoto zinazowakabili watu
wake, jambo linalohitaji kuwekeza zaidi katika elimu na majiundo makini kwa vijana
wa kizazi kipya, ili kuendeleza tunu msingi za maisha kama zilivyoasisiwa na waanzilishi
wa Jumuiya ya Ulaya. Kuna vijana zaidi ya millioni 75 Barani Ulaya ambao hawana fursa
za ajira wala nafasi ya kuweza kujiendeleza kutokana na ukata. Ni hali ambayo inatisha
kwani umaskini wa hali na kipato unaendelea kuongezeka siku hadi siku Barani Ulaya;
mambo yanayotishia: haki, amani na utulivu.
Umoja wa Ulaya unapata chimbuko
lake kutoka katika tunu msingi za maisha ya Kikristo; changamoto ya kuendelea kutoa
kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu, uhuru wa kweli, demokrasia,
usawa na utawala wa sheria. Kanisa bado linadhamana ya kuchangia katika ustawi na
maendeleo ya Bara la Ulaya kwa kujikita katika majadiliano ya kina kati ya imani na
uwezo wa mwanadamu kufikiri na kutenda, dhamana iliyotiliwa mkazo sana na Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto XVI; ili kushirikiana na kushikamana kwa ajili ya ustawi na maendeleo
ya wengi.
Baba Mtakatifu wakati wa ziara yake ya kikazi huko mjini Strasbourg
atakutana na wabunge wa Ulaya pamoja na kuzungumza na Baraza la Ulaya linalounganisha
mataifa 47; kila kundi linatarajiwa kupewa changamoto maalum na umuhimu wa kushikamana
kwa pamoja, ili kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani pamoja na kuendeleza haki
msingi za binadamu, kama vikolezo maalum vya ujenzi wa Bara la Ulaya.
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.