Maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani kwa mwaka 2014 kitaifa yanatarajiwa kufanyika
mkoani Njombe kuanzia tarehe 24 mwezi huu hadi tarehe Mosi Desemba, 2014, kilele cha
maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani. Hayo yamesemwa Jumamosi tarehe 22 Novemba 2014
na Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Taifa ya kudhibiti UKIMWI (TACAIDS) Dkt. Fatma Mrisho
wakati akiongea na waandishi wa habari katika ukumbi wa mikutano uliopo makao makuu
ya tume hiyo jijini Dar es Salaam.
Dkt. Mrisho alisema kauli mbiu ya maadhimisho
hayo ni “Tanzania bila maambukizo mapya ya Virusi Vya Ukimwi (VVU), Vifo vitokanavyo
na UKIMWI, Ubaguzi na unyanyapaa inawezekana”. “Kauli mbiu hii inalenga kutoa msukumo
wa utekelezaji wa mikakati mbalimbali ya kudhibiti UKIMWI kitaifa na kimataifa ili
kufikia azma ya sifuri tatu zinazomaanisha maambukizi mapya sifuri, vifo vitokanavyo
na UKIMWI sifuri na unyanyapaa sifuri ifikapo mwaka 2018”.
Kauli mbiu hii pia
inahimiza utekelezaji wa dhati wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia na maazimio yaliyowekwa
kwenye mkutano maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu UKIMWI uliofanyika mwaka 2001 nchini
Marekani”, alisema Dkt. Mrisho. Alisema kipaumbele cha maadhimisho ya mwaka huu ni
upimaji wa hiari wa VVU na ushauri nasaha, na kutoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa
wingi ili wapate huduma hii muhimu.
Aidha Mkurugenzi huyo aliwataka wananchi
kuadhimisha siku hiyo kwa njia ya makongamano, kumbukumbu za waliofariki kwa UKIMWI,
midahalo, mikutano ya wazi, vipindi kupitia vyombo vya habari, kutembelea na kutoa
misaada kwa watoto yatima na wanaougua ugonjwa huo na kutoa elimu inayohusu kujikinga
na maambukizi.
Akizungumzia kuhusu upatikanaji wa dawa za kupunguza makali
ya ugonjwa wa UKIMWI Mkurugenzi wa Sera, Mipango na Utafiti wa TACAIDS Dkt. Raphael
Kalinga alisema dawa hizo hutolewa bila malipo kwa wahitaji wanaostahili kuzipata
hii ni kulingana na mfumo wa utoaji kwa wahitaji. “Kuna baadhi ya wagonjwa hulazimisha
kupewa dawa za kupunguza makali ya virusi vya UKIMWI ingawa kinga zao bado zinamudu
kukabiliana na tatizo hilo wakati si sahihi kufanya hivyo. Kwani wanaostahili kupata
dawa hizo ni wale ambao kinga zao zipo chini”,alisema Dkt. Kalinga.
Maadhimisho
ya wiki hiyo yataenda sambamba na maonyesho ya shughuli za wadau wa udhibiti UKIMWI
nchini na kongamano la kitaifa la kutathimini hali na mwelekeo wa udhibiti wa ugonjwa
huo.