Jifungeni kibwebwe ili kupata tiba na vifaa tiba kwa ajili ya kuzuia na kuponya ugonjwa
wa mtindio wa ubongo!
Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya, Jumamosi
tarehe 22 Novemba 2014 limehitimisha mkutano wake wa ishirini na tisa uliokuwa unajadili
jinsi ya kuwahudumia wagonjwa wenye mtindio wa ubongo, ili kuwajengea tena matumaini.
Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, anasema Baraza lake la Kipapa limeandaa mkutano
huu, ili kukabiliana vyema zaidi na changamoto zinazoibuliwa katika ugonjwa huu. Kilele
cha mkutano huu ni pale wadau walipokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko
kwenye Ukumbi wa mikutano wa Paulo VI ulioko mjini Vatican.
Baba Mtakatifu
katika hotuba yake, anawashukuru wadau mbali mbali kwa kupembua kwa kina na mapana
tema hii ambayo inagusa wengi; tema ambayo imewapatia wajumbe fursa ya kusali na kusikiliza
shuhuda mbali mbali zilizotolewa na wagonjwa, familia na vyama vya kitume, changamoto
kubwa kwa Serikali, Wataalama na Kanisa katika ujumla wake kuhakikisha kwamba, wanawasaidia
waathirika wa ugonjwa wa mtindio wa ubongo kwa kuthubutu kukutana nao, kuwakaribisha,
kuwaonjesha upendo na mshikamano unaobubujika matumaini mapya, ili kuondokana na unyanyapaa
wanaokumbana nao, mambo yanayochangia usumbufu mkubwa kwa wagonjwa na familia zao.
Kanisa
linapenda kuwasindikiza wagonjwa hawa kwa kusikiliza kwa makini matatizo yanayotokana
na ugonjwa wao, ili wagonjwa na familia zao, waweze kuipokea hali hii bila kuona aibu
au kutumbukia kwenye upweke hasi. Ili kuwasaidia wagonjwa hawa kuna haja ya kujenga
mtandao katika maeneo husika ili kutoa huduma makini inayowahusisha watu wengi zaidi
na wala si wazazi peke yao, kwani kundi hili linaweza kuwaondolea mawazo na hali ya
kuchanganyikiwa.
Baba Mtakatifu Francisko ametumia fursa hii kuwapongeza wadau
mbali mbali wanaoendelea kutoa huduma ili kuwasaidia wagonjwa wenye mtindio wa ubongo
na familia zao. Anaendelea kuwahimiza watalaam, mabingwa na watafiti kujifunga kibwebwe
ili kuhakikisha kwamba, wanapata haraka iwezekanavyo tiba na vifaa tiba, ili kuponya,
lakini zaidi kukinga watoto kutokana na ugonjwa huu. Yote haya yafanyike kwa kuzingatia
haki msingi za mgonjwa, mahitaji yao msingi na nguvu walizonazo, daima utu na heshima
ya binadamu vikipewa kipaumbele cha kwanza.
Baba Mtakatifu Francisko kwa namna
ya pekee amemkumbuka na kumwombea Kardinali Fiorenzo Angelini, aliyefariki dunia mjini
Roma akiwa na umri wa miaka 98. Kardinali Angelini ni muasisi wa Baraza la Kipapa
la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya.
Na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.