2014-11-21 08:47:26

Wagonjwa wa mtindio wa ubongo, wahudumiwe ndani ya familia!


Mkutano wa ishirini na tisa wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya, umefunguliwa rasmi tarehe 20 Novemba 2014, kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Kardinali George Pell, Mwenyekiti wa Sekretarieti ya Kipapa kwa ajili ya uchumi.

Wajumbe wanaendelea kukazia umuhimu wa kutafuta tiba ya ugonjwa wa mtindio wa ubongo kuanzia ndani ya Familia, kwa kushirikiana na wataalam, watafiti na mabingwa katika sekta ya afya, ili kuwajengea matumaini wagonjwa wa mtindio wa ubongo ambao kwa sasa wanakadiriwa kuwa ni asilimia moja ya idadi yote ya watu duniani. Ni ugonjwa unaoacha madhara makubwa kwa mgonjwa, familia na jamii katika ujumla wake, ili kuwajengea matumaini pasi na kukata tamaa.

Wajumbe wamesikiliza shuhuda mbali mbali zilizotolewa na wagonjwa pamoja na familia zao, jinsi ambavyo wanajitahidi kuwahudumia kwa imani na mapendo; kwani familia ni mahali murua zaidi katika kuwahudumia wagonjwa wenye mtindio wa ubongo. Bibi Beatrice Lorenzin, Waziri wa Afya nchini Italia amewaambia wajumbe kwamba, idadi ya wagonjwa wa mtindio wa ubongo inaongezeka maradufu Barani Ulaya na kwamba, kampeni dhidi ya ugonjwa huu inakwamishwa na imani potofu kwamba, mtindio wa ubungo unasababishwa na chanjo zinazotolewa kwa watoto wadogo.

Wataalam na mabingwa wa ugonjwa huu, wanakazia kwamba, kuna haja ya kufanya utafiti wa kina kuhusu chanzo cha ugonjwa huu na umuhimu wa familia kuwahudumia watu wenye ugonjwa huu, wakiwa ndani ya familia badala ya kuwatelekeza. Lengo ni kufuatilia maendeleo ya mgonjwa, kwa uchunguzi na tiba zaidi. Mkutano huu unafungwa rasmi, Jumamosi, tarehe 22 Novemba 2014 kwa kukutana na kusherehekea kwa pamoja na Baba Mtakatifu Francisko.







All the contents on this site are copyrighted ©.