2014-11-21 09:03:58

Kanuni maadili inalenga kudumisha utu wa binadamu na mafao ya wengi!


Jimbo Kuu la Verona, Italia kuanzia tarehe 20 hadi tarehe 23 Novemba 2014 linaadhimisha Tamasha la nne la Mafundisho Jamii ya Kanisa, linaloongozwa na kauli mbiu "Nje ya mahali na ndani ya nyakati", changamoto ya kuhakikisha kwamba, Kanisa linasaidia kutibu na kuganga madonda na machungu ya watu wasiokuwa na fursa za ajira, ili kuwarudishia tena hadhi na utu wao kama binadamu. Tatizo kubwa linalojitokeza ni kufumbia macho na masikio mahangaiko ya watu wasiokuwa na ajira.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa njia ya video katika kongamano hili anasema kwamba, kanuni maadili inayofundishwa na Mama Kanisa inapania pamoja na mambo mengine, kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao ya wengi na huduma kwa jirani, ili kila mtu aweze kufurahia matunda ya kazi ya uumbaji. Wafanyabiashara na wachumi, wanakumbushwa kwamba, fedha ni kwa ajili ya kumhudumia mwanadamu na kamwe isiwe ni chanzo cha nguvu ya kiuchumi na nyanyaso kwa maskini.

Baba Mtakatifu anasema kuna malalamiko mengi kwamba mipango mingi ya maendeleo na utunzaji wa mazingira haiwezi kutekelezeka kutokana na ukata pamoja na hali mbaya ya uchumi, lakini bado kuna kiasi kikubwa cha fedha kinachopatikana kwa ajili ya kununulia silaha zinazoleta maafa na majanga katika maisha ya watu. Lakini pesa peke yake haiwezi kuchochea maendeleo, bali mwanadamu anayeitumia fedha hii kwa hekima na busara anaweza kuwa ni kikolezo kikuu cha maendeleo, kumbe kuna haja ya kuwa na wajasiriamali wanaothubutu kuwekeza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya jamii zao.

Wajasiriamali wanapaswa kuwekeza katika teknolojia, lakini zaidi kwa kuboresha mahusiano ya watu, ili watu wengi zaidi waweze kushiriki huku wakiongozwa na kanuni ya mshikamano kati ya watu, ili kwa pamoja kuweza kutafuta suluhu ya matatizo na changamoto zinazojitokeza, ili kuthamini utu wa watu na kuwawezesha kujitegemea wenyewe, ili kuwa na matumaini ya kesho iliyo bora zaidi. Huu ni mchakato wa maendeleo unaojikita katika upendo na mshikamano, ili kujibu changamoto za kijamii.

Baba Mtakatifu anasema, kuna haja ya kufanya mabadiliko katika maisha, kwa kuwashirikisha wengine ule upendo unaobubujika kutoka katika undani wa maisha ya mtu pamoja na kutumia karama na vipaji alivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya mafao na ustawi wa wengi. Hapa watu watumie akili, ujuzi, maarifa na uwezo kwa ajili ya wengi na kuondokana na tabia ya uchoyo na wivu usiokuwa na mashiko; mambo yanayopelekea watu kutojiamini na hatimaye kuanza kudhaniana vibaya. Umwilishaji wa karama ni chemchemi ya furaha na matumaini makubwa miongoni mwa vijana.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, kuna idadi kubwa ya vijana ambao hawana fursa za ajira, mwaliko kwa wadau mbali mbali kutumia muda waliopewa na Mwenyezi Mungu, ili kushirikishana hazina ambayo wamekabidhiwa na Mungu, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi, ili kupata utimilifu wa maisha ya binadamu. Baba Mtakatifu anawashukuru viongozi wa Jimbo Kuu la Verona kwa kujielekeza zaidi katika kuunda dhamiri nyofu zinazoelewa changamoto za kijamii na ufumbuzi wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.