2014-11-21 09:44:10

Jitokezeni kuchukua formu na kushiriki uchaguzi wa Serikali za mitaa


Serikali ya Tanzania imesema kuwa itatumia jumla ya shilingi bilioni 20 kwa ajili ya matumizi ya zoezi la uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Desemba mwaka 2014 hadi kukamilika. Gharama hizo zimetolewa na Mkurugenzi wa Idara ya Serikali za Mitaa Ofisi ya Waziri Mkuu Tamisemi, Kharist Luanda, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Dodoma. Alisema kuwa gharama hizo zinajumuisha tangu kuanza kwa zoezi mzima la maandalizi ya uchaguzi huo wa serikali za mitaa mpaka siku ya upigaji wa kura utakapokamilika.

Alisema kuwa gharama zingine ambazo zitakazotumika kwenye matumizi ya fedha hizo,ni pamoja fedha za kusafirisha masanduku,posho,usafiri,kulipa wasimamizi wa uchaguzi huo na semina mbalimbali zilizokuwa zikitolewa kwa ajili ya elimu. Akizungumza kuhusu zoezi la uandikishaji wa wapiga kura alisema kuwa bado watanzania hawana mwitikio wa kujitokeza katika kujiandikisha na kuchukua fomu za kugombea, hivyo amewataka kujitokeza ili waweze kutimiza haki yao ya kuwapata viongozi wanaokubarika.

Alisema kwa kufanya hivyo wataepukana na kupiga makelele na tabia ya kuchaguliwa viongozi kutokana na kutojitokeza ambako watanzania wengi wameshindwa kutumia haki yao hiyo.

Mkurugenzi huyo aidha alifafanua kuwa uandikishaji wa wapiga kura wa mwaka huu wa 2014 katika chaguzi zake za serikali za mitaa utafanyika kwa kutumia Daftari la wakazi badala ya kutumia daftari ya kudumu ya wapiga kura inayotumika kwa viongozi wa ngazi ya udiwani,wabunge hadi Rais.

Luanda alisema kuwa uandikishaji huo wa wapiga kura kwa mwaka huu pia utafanyika kwenye majengo ya umma na pale ambapo itaonekana hakuna jengo la umma,basi utafanyika katika sehemu ambayo wasimamizi wa uchaguzi watakubaliana na viongozi wa vyama vya siasa. Hata hivyo Mkurugenzi huyo alisema kuwa zoezi la kuanza kuchukua fomu za kugombea litaanza tarehe, 23-29 /11 mwaka huu,hivyo akawataka wale wote watakaogombea kupitia vyama vyao vya siasa wafike kwenda kuchukua fomu kwa wasimamizi wa vituo.

“Ninaomba wagombea watakapochukua fomu hizo wahakikishe wanasoma maelekezo kwa makini, ili kuepuka kuwekewa pingamizi na wagombea wengine kwa madai kukiuka ujazaji wa fomu hizo vibaya”alisema. Mkurugenzi huyo kuhusu nembo zitakazotumika kwenye fomu ya kugombea kwenye chaguzi hizo, alisema kuwa kila fomu itakuwa na nembo ya Halmashauri husika na nembo ya chama cha siasa chenye wagombea.








All the contents on this site are copyrighted ©.