2014-11-20 08:13:32

Kilimo kwanza nchini Tanzania na mafanikio yake!


Baa la njaa ni matokeo ya ukosefu wa sera makini katika mikakati ya uzalishaji, ugavi na masoko; ni kielelezo cha ubinafsi unaowafanya baadhi ya watu kufaidika zaidi kwa kula na kusaza na hata pengine kumwaga chakula hiki, wakati kuna maelfu ya watu wanakufa kwa baa la njaa sehemu mbali mbali duniani. Kuna haja ya kuwa na sera makini katika sekta ya kilimo ili kuwa na uhakika wa usalama wa chakula kinachokidhi viwango vya kimataifa ili kukabiliana pia na lishe duni. RealAudioMP3

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Dr. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano wa kimataifa kuhusu lishe ulioandaliwa na Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa anasema kwamba, Sera ya Kilimo kwanza inaendelea kupata mafanikio makubwa nchini Tanzania kutokana na ongezeko la uzalishaji wa mazao ya chakula kiasi kwamba kwa sasa Tanzania ina ziada ya chakula kwa asilimia 20%.

Sera ya Kilimo kwanza imepata mwitikio mkubwa kwani watanzania wengi kwa sasa wanatumia pembejeo za kisasa katika uzalishaji, kiasi kwamba, Serikali inaanza kujipanga ili kujenga maghala makubwa kwa ajili ya kuhifadhi nafaka zinazozalishwa na wakulima sehemu mbali mbali za nchi.

Serikali inaendelea kuboresha mfumo wa masoko, ili wakulima waweze kuwa na uhakika wa soko la mazao wanayoyazalisha, kwa kuwa na mfumo wa kubadilishana mazao sokoni. Zoezi hili limepata mafanikio makubwa nchini Ethiopia na Serikali ya Tanzania inasema, inataka kuona mafanikio haya pia kwa wakulima wake. Dr. Bilal anasema, mafanikio ya Sera ya Kilimo kwanza ni kutaka kuharakisha ustawi na maendeleo ya wakulima wengi nchini Tanzania kwa kuwa na uhakika wa chakula.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.