2014-11-20 11:24:14

Injili ya Uhai ni matunda ya mkamilishano kati ya Bwana na Bibi!


Mkamilishano kati ya Bwana na Bibi, daima limekuwa ni jambo ambalo linavuta hisia za watu wengi, kiasi hata cha kuwaacha watu wakiwa wamshikwa na bumbuwazi. Huu ni mkamilishano usiofungwa na mambo ya fedha na biashara, bali katika upendo unaobubujika kutoka katika undani wa mtu.

Haya ndiyo yaliyojiri katika kongamano la kimataifa la majadiliano ya kidini lililoandaliwa na Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa kwa kushirikiana na Mabaraza mengine ya Kipapa ili viongozi wa kidini kuweza kujadili mkamilishano kati ya Bwana na Bibi, tangu tarehe 17 hadi tarehe 19 Novemba 2014 hapa mjini Vatican. Itakumbukwa kwamba, kongamano hili lilifunguliwa na Baba Mtakatifu aliyekazia umuhimu wa watoto kupata wazazi wote wawili, yaani Baba na Mama na wala si vinginevyo.

Kongamano hili limewashikirisha viongozi mbali mbali wa kidini, ambao kwa pamoja wamekiri ukuu na umuhimu wa maisha ya ndoa na familia kadiri ya mpango wa Mungu. Bwana na Bibi kwa hiyari yao wenyewe wanaamua kufungamana katika maisha; katika raha na shida; katika afya na magonjwa, wakipendana na kuheshimiana siku zote za maisha yao. Mkamilishano huu ni chemchemi ya maisha mapya na mwendelezo wa jamii ya binadamu.

Wajumbe wa kongamano la mkamilishano kati ya Bwana na Bibi wanatambua mchango mkubwa unaoweza kutolewa na ndugu, jamaa na marafiki kwa wanandoa wapya katika hija ya maisha yao ya kila siku, kwa njia ya mifano bora ya maisha na ushauri mwanana, lengo likiwa na kudumisha maisha ya ndoa na familia. Hili ni kundi ambalo linakuwa la kwanza kufaidika na ndoa dumifu, kwani wamewekeza kwa dhati katika ustawi na maendeleo ya wanandoa wenyewe.

Muungano kati ya Bwana na Bibi unapania kuendeleza Injili ya Uhai kwa binadamu na tamaduni zake, lakini ni taasisi inayokabiliwa na changamoto nyingi na tete. Ndoa za uhakika zisizofungamana na "mshiko" zinaendelea kupungua na kwamba, upendo umegeuzwa kuwa bidhaa na chombo cha kampeni inayokumbatia utamaduni wa kifo. Ndoa ni mahali ambapo, binadamu anawekeza kwa ajili ya Injili ya Uhai!







All the contents on this site are copyrighted ©.