2014-11-19 08:27:53

Kila mtu anawajibika kutumia vyema karama zake!


Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumapili iliyopita amehitimisha ziara ya kikazi nchini Czech, kwa mwaliko wa Kardinali Dominik Duka, kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka 25 tangu Agnese wa Bohemia, alipotangazwa kuwa Mtakatifu, kwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa la Mtakatifu Yohane Paulo II, aliyemtangaza Agnese kuwa mtakatifu hapo tarehe 12 Novemba 1989.

Kardinali Parolin, wakati wa mahubiri yake amemtaja Mtakatifu Agnese kuwa ni mtu anayependwa na kuthaminiwa na waamini wengi, kwani kutangazwa kwake kuwa Mtakatifu kilikuwa ni kiashilia cha kuanguka kwa utawala wa Kikomunisti nchini Czech na hapo ukawa ni mwanzo wa mchakato wa demokrasia ya kweli na ujenzi wa umoja na mshikamano wa kitaifa. Jubilee ya Mtakatifu Agnese imekwenda sanjari na kumbu kumbu ya miaka ishirini na mitano ya kuanguka kwa utawala wa Kikomunisti.

Mtakatifu Agnese alikuwa na upendo mkubwa kwa maskini na wote waliokuwa wanateseka kwa magonjwa na umaskini, mwaliko kwa waamini kukesha na kuhakikisha kwamba, wanatumia vyema karama zao kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa na Jamii inayowazunguka, kwa kutambua kwamba, kila mtu anawajibika kukuza na kuendeleza karama ili ziweze kuzaa matunda yanayokusudiwa.

Waamini wamepewa karama hizi kwa ajili ya mafao ya wengi na wala si kwa ajili ya matumizi ya mtu binafsi peke yake. Kardinali Parolin amewataka waamini kutumia karama na vipaji vyao kwa ajili ya kushikamana na wale wote wanaosimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu, kwani Kristo anahamasishwa kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko, kutoka na kuwaendea wengine ili kuwashirikisha Injili ya Furaha na Matumaini.







All the contents on this site are copyrighted ©.