Hija ya kichungaji huko Strausbourg na Uturuki ni za kihistoria!
Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kutembelea Makao makuu ya Umoja wa Ulaya huko
Strausbourg hapo tarehe 25 Novemba 2014, hii ikiwa ni hija yake ya tano kimataifa
na tarehe 28 hadi 30 Novemba 2014 atafanya hija ya kiekumene nchini Uturuki; matukio
ambao yana umuhimu wa pekee anasema Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican
wakati alipokuwa anazungumza na waandishi wa habari mjini Vatican Jumatatu tarehe
17 Novemba 2014.
Ni kwa mara ya kwanza matukio haya yanafanyika katika kipindi
kifupi kutokana na kalenda ilivyokaa kwa ajili ya Wabunge wa Bunge la Ulaya na Maadhimisho
ya Siku kuu ya Mtakatifu Andrea, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 30 Novemba.
Patriaki Bartolomeo wa kwanza amemwalika Baba Mtakatifu Francisko kushiriki katika
maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Andrea kwa mwaka huu, ili kuendeleza hija ya
kiekumene, iliyoanzishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.
Padre
Lombardi anasema, hija ya Baba Mtakatifu mjini Strausburg itakuwa ni fupi sana kuwahi
kufanywa na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni hija itakayodumu muda wa masaa manne tu,
ambayo Baba Mtakatifu Francisko atapata nafasi ya kuhutubia Bunge la Ulaya pamoja
na kuhutubia pia Baraza la Ulaya. Hii ni safari ya kikazi na wala haina uhusiano wowote
na masuala ya kidini au maisha ya kiroho. Baba Mtakatifu anakwenda kuhutubia huko
kwani Jumuiya ya Kimataifa inatambua dhamana na utume wake wa kimaadili na ndiyo maana
vyombo hivi vina mahusiano ya kidiplomasia na Vatican.
Akiwa mjini Strausburg,
Baba Mtakatifu atapata fursa ya kuzungumza na viongozi wa ngazi ya juu wa taasisi
hizi za kimataifa kwa kugusia: matatizo, wajibu na changamoto zinazolikabili Bara
la Ulaya. Kwa mara ya mwisho, Mtakatifu Yohane Paulo II alihutubia taasisi hizi kunako
mwaka 1988, wakati huo bado Ukuta wa Berlin, kielelezo cha siasa za chuki na uhasama
ukiwa bado umesimama.
Padre Lombardi anasema, hija ya kiekumene ya Baba Mtakatifu
Francisko nchini Uturuki ni mwendelezo wa hija ambazo zimewahi kufanywa na Mababa
Watakatifu kama vile: Yohane XXIII, Paulo VI, Yohane Paulo II na Baba Mtakatifu Mstaafu
Benedikto XVI. Baba Mtakatifu Francisko atakapowasili nchini Uturuki atakutana na
kuzungumza na viongozi wa Serikali na Wanadiplomasia.
Jumamosi, tarehe 29
Novemba, 2014, itakuwa ni siku maalum kwa ajili ya majadiliano ya kiekumene na udugu
kati ya Wakristo na Waislam. Baba Mtakatifu atatembelea Makumbusho ya Sofia yanayofumbata
mahusiano kati ya dini ya Kiislam na Kikristo. Atatembelea Msikiti mkuu wa Instanbul
na baadaye Baba Mtakatifu atakutana na wawakilishi wa Jumuiya za Kikristo na baadaye
jioni ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Roho Mtakatifu.
Jumapili,
tarehe 30 Novemba 2014 baada ya kusalimiana na Rabi mkuu wa Uturuki, Baba Mtakatifu
atashiriki katika Ibada Takatifu ya Kiekumene kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu George,
kama sehemu ya maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Andrea. Katika tukio, viongozi
hawa wawili watatoa tamko la pamoja kuhusiana na mchakato wa majadiliano ya kiekumene.