Papa amtembelea Kardinali Jorge Maria Mejia aliyelazwa hospitalini!
Baba Mtakatifu Francisko mara tu baada ya tafakari ya Sala ya Malaika wa Bwana kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 16 Novemba
2014 aliondoka mjini Vatican kuelekea Castel Gandolfo, nje kidogo ya Roma, ili kuzindua
sanamu ya chuma iliyotengenezwa na Msanii maarufu kutoka Argentina, Bwana Alejandro
Marmo.
Katika safari, Baba Mtakatifu aliambatana na viongozi kadhaa kutoka
Vatican, akabahatika kukutana na kuzungumza kwa kitambo kidogo na kikundi cha wananchi
kutoka Argentina wanaofahamiana naye waliokuwa mjini Castel Gandolfo. Baadaye Baba
Mtakatifu aliendelea na shughuli ya kubariki sanamu hizo.
Baadaye jioni wakati
alipokuwa anarejea mjini Vatican, Baba Mtakatifu alikwenda kumtembelea Kardinali Jorge
Maria Mejia, aliyelazwa kwenye Kliniki ya Pio wa Kumi na moja. Aliporejea mjini Vatican
alikwenda moja kwa moja kusalimiana na vijana wanaoshiriki katika kongamano la kimataifa
katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu na baadaye akarejea kwenye Makao
yake yaliyoko kwenye Hosteli ya Mtakatifu Martha, mjini Vatican.