Msifungie talanta zenu masandukuni, zitumieni kwa mafao ya wengi!
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa tafakari kwa Sala ya Malaika wa Bwana, kwenye Uwanja
wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumapili tarehe 16 Novemba 2014 amekumbusha
kwamba, Mwenyezi Mungu amemkirimia kila mwanadamu karama na mapaji maalum ambayo anapaswa
kuyatumia kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi na wala karama hizi hazipaswi
kufungiwa masandukuni.
Baba Mtakatifu anasema, Mwenyezi Mungu amewakirimia
waamini karama ya: Neno. Ekaristi Takatifu, Imani, Upendo na Msamaha, mambo muhimu
katika maisha ya mwamini, ambayo anapaswa kuyatumia ili yaweze kuzaa matunda yanayokusudiwa.
Waamini wanapaswa kuondokana na woga usiokuwa na mashiko kwa kuhakikisha kwamba, karama
zao zinazaa matunda kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.
Huruma, wema
na msamaha ni mambo ambayo Yesu mwenyewe anawakirimia wafuasi wake, ili waweze kuyatumia
kwa ajili ya jirani zao, katika mazingira na medani mbali mbali za maisha; jambo la
msingi ni kuhakikisha kwamba, Wakristo wanatolea ushuhuda wenye mashiko kuhusiana
na imani yao, katika ukweli na uwazi.
Baba Mtakatifu anasema, Neno la Mungu
linawahamasisha waamini kushuhudia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake na kamwe wasizike
Injili, bali wahakikishe kwamba, wanaitangaza kwa njia ya ushuhuda unaojikita katika
uhalisia wa maisha. Hii ni nguvu inayoweza kumweka mtu katika mahangaiko, lakini inasafisha
na kupyaisha maisha ya mwamini.
Baba Mtakatifu anakazia kwa namna ya pekee
kabisa umuhimu wa waamini kujikita katika Msamaha unaotolewa na Kristo kwa njia ya
Sakramenti ya Upatanisho. Sakramenti hii ni muhimu sana kwani inawasaidia waamini
kuvunjilia mbali kuta za ubinafsi zinazopelekea mahusiano tenge, ili kuanza mchakato
wa majadiliano, ambayo yatasaidia kukuza na kudumisha mawasiliano kati ya watu. Mwenyezi
Mungu anatambua uwezo wa kila mtu na hivyo kumkirimia kadiri ya nafasi na haki ya
Mungu.
Mwenyezi Mungu ana matumaini na wajawake, kamwe waamini wasimkatishe
tamaa, wala kumdanganya kwa woga usiokuwa na mashiko, bali kulipa matumaini yanayoonesha
matumaini ya kweli.
Baba Mtakatifu anasema, Bikira Maria alibahatika kupata
zawadi kubwa na nzuri kuliko zote, yaani Yesu, Mwana wa Mungu; akamkirimia ubinadamu
kwa kumwonjesha moyo wenye ukarimu na mapendo. Basi waamini wamwombe Bikira Maria
ili aweze kuwajalia kuwa kweli ni watumishi wema na waaminifu, ili waweze kushiriki
kikamilifu katika furaha ya Bwana wao.
Baba Mtakatifu Francisko, mwishoni
amewataka waamini kusoma mfano wa talanta katika Injili kama ilivyoandikwa na Mathayo:
25:14- 30. Kila mwamini achunguze dhamiri yake ili kuona kama kweli zawadi alizokirimiwa
na Mwenyezi Mungu, zinatumika kwa ajili ya mafao ya wengi au zinabinafishwa kwa ajili
ya mafao ya mtu binafsi?
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.