2014-11-17 12:14:13

Jitokezeni kwa wingi kuzungumzia mustakabali wa Tanzania kwa kukutana na Makamu wa Rais


Dr. James Msekela Balozi wa Tanzania nchini Italia, Jumapili tarehe 16 Novemba 2014 alipata nafasi ya kuzungumza na Jumuiya ya Wanafunzi Watanzania Wakatoliki pamoja na Watanzania wanaoishi mjini Roma, baada ya kuhudhuria Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kuombea amani, ustawi na maendeleo nchini Tanzania. RealAudioMP3

Dr. Msekela amewaambia watanzania kwamba, Dr. Mohamed Gharib Bilal anatarajiwa kuzungumza na watanzania wanaoishi nchini Italia siku ya tarehe 18 Novemba 2014 kwenye Ukumbi wa Hotel ya Ambasciatori Palace, iliyoko kwenye mtaa wa Vittorio Veneto namba 62, majira ya saa 9:00 Alasiri. Makamu wa Rais atakuwa mjini Roma ili kuhudhuria mkutano wa pili wa lishe kimataifa ambao umeandaliwa na Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani, WHO, ili kuweka mikakati ya kupambana na baa la njaa pamoja na lishe duni duniani.

Dr. Msekela anasema, awali, FAO ilikuwa imemwalika Rais Jakaya Kikwete, lakini kutokana na sababu zisizozuilika hakuweza kuhudhuria katika mkutano huu muhimu wa Kimataifa na badala yake, FAO imeendelea kuheshimu maamuzi yake na hivyo Makamu wa Rais Dr. Mohamed Gharib Bilal anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mkutano huu wa Lishe Kimataifa unafanyika tena baada ya kupita takribani miaka 22 iliyopita. Watanzania wanaoishi nchini Italia watapata nafasi ya kumsikiliza na kuzungumza na Makamu wa Rais kuhusiana na masuala mbali mbali yanayohusu ustawi na maendeleo ya watanzania wote, hasa wakati huu Tanzania inapojiandaa kukabiliana na changamoto ngumu kuhusiana na: chaguzi za Serikali za mitaa, Kura ya maoni na uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika kunako mwaka 2015.

Dr. Msekela ameipongeza pia Radio Vatican kwa kusaidia kuwahamasisha watanzania kuhudhuria tukio hili kwa njia ya tovuti na matangazo yake. Ni matumaini ya Balozi wa Tanzania nchini Italia kwamba, licha ya shughuli nyingi walizonazo watanzania, lakini walau wataweza kutenga muda ili kuweza kukutana na Makamu wa Rais kwa ajili ya mustakabli wa Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.