Washirikisheni wengine amani inayofumbatwa katika upendo, wema, uaminifu na furaha!
Mama Kanisa anafundisha kwamba, amani ni kitu chenye thamani kubwa na zawadi ya pekee
kutoka kwa Mwenyezi Mungu ambaye ndiye asili ya zawadi hii. Amani ina msingi wake
katika uelewa sahihi wa binadamu, wenye msingi unaojikita katika haki na upendo. Ikumbukwe
kwamba, amani ni tunda la haki; amani pia ni tunda la mapendo. Amani kimsingi hujengwa
siku hadi siku kwa kutafuta muafaka kadiri ya mpango wa Mungu pamoja na kutambua kwamba,
kila mmoja anawajibika kulinda, kudumisha na kutetea amani.
Vurugu na kinzani
si jibu muafaka la kutafuta amani ya kweli na kutafuta ufumbuzi wa matatizo na changamoto
anazokabiliana nazo binadamu. Ulimwengu mamboleo unahitaji mashuhuda na wajenzi wa
misingi ya amani, ili kulinda na kudumisha haki msingi za binadamu; kwa kutoa ushuhuda
wa upendo hasa kwa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii na kwamba, vurugu na kinzani
ni mchakato unaopania kuendeleza utamaduni wa kifo!
Baba Mtakatifu Francisko
katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii anabainisha kwamba, Mkristo,
kimsingi anapaswa kuwapelekea wengine zawadi ya amani. Akiwa na zawadi hii anapaswa
pia kuwamegea na kuwashirikisha wengine upendo, wema, uaminifu na furaha!