2014-11-13 10:48:35

Vita inaharibu, inaua na kuwatumbukiza watu katika umaskini!


Kanisa linaichangamotisha Jumuiya ya Kimataifa kuangalia dhana ya vita katika mwelekeo mpya, ili kudumisha misingi ya haki, amani, ustawi na maendeleo ya binadamu. Vita ni balaa na njia isiyofaa kwa kutatua na kumalizamatatizo yanayozuka kati ya mataifa. Vita inatabia ya kuzua migogoro na kinzani mpya na zenye utata zaidi. Vita inapozuka husababisha mauaji ya kinyama yasiyo ya lazima na kwamba, ni tukio ambalo linahatarisha hali ya maisha ya binadamu kwa sasa na kwa siku za usoni.

Mababa wa Kanisa wanafundisha kwamba, hakuna kinachoweza kupotea kwa kuwa na amani, lakini kinyume chake ni kwamba kila kitu kinaweza kupotea kwa vita. Madhara ya mapambano ya silaha yanamgusa mtu mzima: kiroho na kimwili na kwamba, vita ni kushindwa kwa utu wa kweli wa binadamu wote. Vita daima ni kushindwa kwa binadamu.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii anasema kwamba, vita inasababisha uharibifu mkubwa, inaangamiza, inawadumbukiza watu katika dimbwi la umaskini, njaa na magonjwa. Baba Mtakatifu anamwomba Yesu Kristo, Bwana wa amani, awajalie walimwengu zawadi ya amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.